Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Majibu kwa Maandamano ya Kupinga Hijab Nchini Iran

(Imetafsiriwa)

Zifuatazo ni baadhi ya nukta muhimu kuhusiana na matukio ya hivi sasa nchini Iran kufuatia kifo cha Mahsa Amini mwenye umri wa miaka 22 ambaye inasemekana aliuawa akiwa chini ya ulinzi wa jeshi la polisi la utawala huo, kutokana na kutovaa Hijabu ipasavyo.

1. Kupigwa hadi kufa kwa Mahsa Amini kulikuwa ni kosa wazi kwa mujibu wa Uislamu ambao unaoharamisha aina yoyote ya mateso. Hili liko wazi katika maandiko ya Kiislamu. Mtume (saw) amesema:

«إِنَّ اللهَ يُعَذِّبُ الَّذِينَ يُعَذِّبُونَ فِي الدُّنْيَا»

“Mwenyezi Mungu huwatesa wale wanaotesa watu duniani.”

2. Kuna watu wengi masekula wanaopatiliza kutumia matukio haya nchini Iran kwa mara nyingine tena kutupa madai yao ya kale ya kiorientalisti na uwongo dhidi ya hijab na sheria za kijamii za Kiislamu, wakiutuhumu kwa urongo Uislamu na Shariah kwa kuwakandamiza wanawake. Kwa mfano, hii ilikuwa ni nukuu ya makala ya mwandishi wa habari Janice Turner katika tovuti ya Times ya Uingereza ya tarehe 23 Septemba, chini ya kichwa, 'Iwapo hijab itaondoka, utawala katili wa Iran utafuata': “Hijab si vazi tu, ni chombo cha udhibiti kilichoundwa kwa ajili ya kutishia na kugawanya taifa zima." Madai haya ya kipuuzi ni kwamba vazi la Kiislamu linasaidia kuwezesha kuendelea kwa utawala wa serikali dhalimu kama vile Iran. Tuhma kama hizo, zilizozaliwa kutokana na mtazamo wa chuki dhidi ya Uislamu, ujinga na mtazamo wa kiulimwengu unaoegemea Ulaya na thaqafa nyenginezo, zinahitaji kupingwa kwa sauti kali.

3. Dhana ya kuwa utawala wa Iran unajali kutabikisha na kulinda sheria za Kiislamu ni ya kipuuzi kwani huu ndio utawala uliomsaidia mchinjaji Assad kuwachinja makumi kwa maelfu ya Waislamu wasio na hatia nchini Syria na ilikuwa na mkono wake katika mauaji ya Waislamu wasio na hatia nchini Iraq na Yemen. Pia imewaua Waislamu wa Afghanistan wanaojaribu kuvuka mipaka yake kutafuta maisha bora. https://www.hizb-ut-tahrir.info/en/index.php/press-releases/afghanistan/19439.html. Mtume (saw) amesema:

«كُلُّ الْمُسْلِمِ عَلَى الْمُسْلِمِ حَرَامٌ؛ دَمُهُ وَمَالُهُ وَعِرْضُهُ»

“Kila Muislamu kwa Muislamu mwengine ni haramu; damu yake, mali yake na heshima yake” (Muslim).

4. Wapo wanaojaribu kuonesha tatizo linalowakabili wanawake nchini Iran kuwa ni utekelezaji wa Hijab na sheria nyingine za kijamii za Kiislamu na ukosefu wa usawa wa kijinsia, ilhali tatizo halisi la Iran likiwa ni kuwepo kwa utawala wa kitheokrasi unaotawala kwa mujibu wa matakwa na maagizo ya watu wa dini - badala ya Qur'an na Sunnah. Mfumo wowote unaotawaliwa na matakwa ya binadamu - demokrasia au udikteta - utasababisha ukandamizaji wa watu na kuwanyimwa haki zao. Mwenyezi Mungu (swt) anasema:

(وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أنزَلَ اللّهُ فَأُوْلَـئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ)  

“Na wasio hukumu kwa yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu, basi hao ndio madhaalimu.” [Al-Maida: 45].

5. Inaeleweka kuwa watu wanakerwa na vitendo vya kidhalimu na vya kimabavu vya utawala wa Iran. Lakini kwa nini baadhi ya wanawake wa Kiislamu katika maandamano haya wanachoma hijab zao na kucheza hadharani, wakionyesha hasira na uasi wao dhidi ya Amri zinazotoka kwa Mwenyezi Mungu (swt) - Mola na Muumba wao? Kufinika mwili mzima wa mwanamke, isipokuwa mikono na uso, mbele ya wanaume wasio Mahram ni faradhi ya Kiislamu iliyofafanuliwa kwa uwazi kabisa na Qur’an na Sunnah, na sio amri kutoka kwa Wairani au utawala wowote mwingine. Mwenyezi Mungu (swt) anasema:

(وَقُل لِّلْمُؤْمِنَاتِ يَغْضُضْنَ مِنْ أَبْصَارِهِنَّ وَيَحْفَظْنَ فُرُوجَهُنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا مَا ظَهَرَ مِنْهَا وَلْيَضْرِبْنَ بِخُمُرِهِنَّ عَلَى جُيُوبِهِنَّ وَلَا يُبْدِينَ زِينَتَهُنَّ إِلَّا لِبُعُولَتِهِنَّ أَوْ آبَائِهِنَّ أَوْ آبَاء بُعُولَتِهِنَّ أَوْ أَبْنَائِهِنَّ أَوْ أَبْنَاء بُعُولَتِهِنَّ أَوْ إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي إِخْوَانِهِنَّ أَوْ بَنِي أَخَوَاتِهِنَّ أَوْ نِسَائِهِنَّ أَوْ مَا مَلَكَتْ أَيْمَانُهُنَّ أَوِ التَّابِعِينَ غَيْرِ أُوْلِي الْإِرْبَةِ مِنَ الرِّجَالِ أَوِ الطِّفْلِ الَّذِينَ لَمْ يَظْهَرُوا عَلَى عَوْرَاتِ النِّسَاء)

“Na waambie Waumini wanawake wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao, wala wasionyeshe uzuri wao isipo kuwa unao dhihirika. Na waangushe shungi zao juu ya vifua vyao, wala wasionyeshe uzuri wao ila kwa waume zao, au baba zao, au baba wa waume zao, au watoto wao, au watoto wa waume zao, au kaka zao, au wana wa kaka zao, au wana wa dada zao, au wanawake wenzao, au iliyo wamiliki mikono yao ya kuume, au wafwasi wanaume wasio na matamanio, au watoto ambao hawajajua mambo yaliyo khusu uke.” [An-Nur: 31]. Na Mtume (saw) amesema,

«إِنَّ الْجَارِيَةَ إِذَا حَاضَتْ لَمْ يَصْلُحْ أَنْ يُرَى مِنْهَا إِلا وَجْهُهَا وَيَدَاهَا إِلَى الْمَفْصِل»

“Pindi msichana anapovunja ungo, haifai aonekane isipokuwa uso wake na viganja vyake vya mikono.” [Imepokewa na Abu Dawud].

6. Kuna wale wanaojaribu kuionyesha Iran kama kielelezo cha jinsi maisha yangekuwa kwa wanawake na watu wengine chini ya utawala wa Kiislamu, huku mfumo wa kisiasa wa kitheokrasi - rais - bunge - nchini Iran, ukiwa na yule anayeitwa 'Kiongozi Mkuu' na kuongozwa na watu wa dini hauna msingi katika maandiko ya Kiislamu. Bali, muundo wa Uislamu wa utawala kama ulivyofafanuliwa kwa uwazi kabisa na Qur'an na Sunnah ni Khilafah kwa njia ya Utume, ambayo ina kiongozi aliyechaguliwa ambaye anawajibika kwa watu, na anatawala pekee kwa mujibu wa Qur'an na Sunnah badala ya maagizo ya watu wa dini waliojiteua wenyewe.

7. Utawala wa Iran ni uongozi wa kimabavu na unahitaji kuondolewa, kama ilivyo kwa tawala zote za sasa zisizo za Kiislamu na za kidikteta katika ardhi za Kiislamu. Hata hivyo, waandamanaji wanaotaka kuwepo kwa mustakbali huria kwa nchi kwa kuamini kwamba hilo litaleta mustakbali mwema kwa wanawake na wengine katika nchi wamepotoshwa sana. Tuzinaona dola za kiliberali katika Magharibi na kwingineko zikitumbukia kutoka kwenye mgogoro mmoja hadi mwingine na matatizo makubwa ya kijamii na kimaadili. Hii ni pamoja na janga la unyanyasaji dhidi ya wanawake pamoja na pia tsunami ya familia zilizovunjika. Mmoja kati ya wanawake watatu katika Muungano wa Ulaya ni muathirika wa unyanyasaji, huku mmoja kati ya wawili wamepitia unyanyasaji wa kijinsia (Tume ya Ulaya). Nchini Ufaransa, mwanamke huuawa kila baada ya siku tatu na mpenzi wa sasa au wa zamani (The Guardian, 2019), huku Marekani, karibu wanawake 3 wanauawa kila siku kupitia unyanyasaji wa kinyumbani (Afisi ya Haki). Haya yote ni matokeo ya maadili ya kiliberali kama vile uhuru wa kibinafsi na wa kijinsia, yanayoshajiisha wanaume kutenda kulingana na matakwa na matamanio yao ya kibinafsi. Pia ni matokeo ya kukosekana kwa sheria za wazi za kijamii za kudhibiti uhusiano kati ya wanaume na wanawake na kufafanua haki na wajibu wao katika maisha ya familia na jamii ili uhusiano wa utu na heshima umakinishwe baina ya jinsia, kwa msingi wa ushirikiano unaofaa. Ni ushirikiano huu unaofaa kati ya wanaume na wanawake ndani ya jamii ambayo sheria za kijamii za Kiislamu, ambapo hijabu ni sehemu yake, zinalenga kuufikia.

8. Njia pekee ya kujenga mustakbali mwema kwa wanawake na watu wengine nchini Iran na kwingineko katika ulimwengu wa Kiislamu ni utabikishaji kamili na sahihi wa Uislamu chini ya Mfumo wa kisiasa wa Mwenyezi Mungu (swt), Khilafah kwa njia ya Utume. Yeyote anayeuchunguza mfumo huu kwa njia yenye malengo, iliyo huru kutokana na ngano na uwongo wa kikoloni, atatambua kwamba una njia ya kuaminika na iliyojaribiwa kwa wakati ya kuweka heshima kwa wanawake ndani ya jamii, kuwalinda dhidi ya unyanyasaji, na kuwadhamini haki zao zote za kisiasa, kiuchumi, kielimu, kisheria na kijamii walizopewa na Mwenyezi Mungu. Hizi ni haki ambazo haziwezi kutupiliwa mbali na watawala, kwani zimefafanuliwa na Mwenyezi Mungu (swt) na hivyo haziwezi kujadiliwa. Hii ni kinyume na dola za kisekula, kama vile Ufaransa, Denmark, Ubelgiji na Uholanzi, ambazo zimewapora wanawake na wasichana wa Kiislamu haki zao za kielimu, kiuchumi na nyinginezo kupitia marufuku zao za hijabu na niqab. Kama Waislamu, tunapaswa kutambua kwamba kamwe hakuwezi kuwa na mafanikio yoyote katika maisha haya au Akherah, isipokuwa kwa kuzikumbatia kwa ukamilifu Sheria na Mfumo wa Muumba wetu, Mwenyezi Mungu (swt) – Mwingi wa hekima, Mjuzi wa yote.

(يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ اتَّقُواْ اللّهَ وَابْتَغُواْ إِلَيهِ الْوَسِيلَةَ وَجَاهِدُواْ فِي سَبِيلِهِ لَعَلَّكُمْ تُفْلِحُونَ)

“Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi Mungu, na tafuteni njia ya kumfikilia. Na wanieni kwa juhudi kwa ajili yake ili mpate kufaulu.” [Al-Maida: 35]

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Dkt. Nazreen Nawaz
Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu