Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Ombwe la Kisiasa Nchini Pakistan

(Imetafsiriwa)

Katika kipindi cha wiki moja tu, kutokana na maagizo ya IMF, serikali ya Pakistan imeongeza bei ya petroli na dizeli kwa PKR 60. Hivyo petroli imechupa kutoka PKR 150 hadi 210! Kwa mara nyengine, mfumo wa uagiziaji umeweka rekodi mpya. Rekodi ya awali iliyowekwa na serikali ya PTI isiyo na ruwaza imevunjwa na serikali ya sasa ya PML-N isiyo na ruwaza, kwa kuongeza bei kwa PKR 60!

Wakati PTI ilipoongeza bei ya petroli katika kipindi chake madarakani kwa maagizo ya IMF, muungano wa upinzani, PDM uliojumuisha PML-N, walisemea juu ya hili. Ukiilaani serikali ya PTI, upinzani uliandaa “Maandamano ya Mehngai Mukao (Mandamano ya Ondoa Mfumko wa Bei)” wakitaka kumaliza upandaji wa bei na kurejesha chini mfumko wa bei. Waliwakusanya watu mabarabarani kwa kauli mbiu tupu, huku wakikosa suluhisho kabisa kwa bei kubwa ya petroli.

Hivi sasa PML-N wapo madarakani, PML-N vilevile, kutokana na maamrisho ya IMF, wameongeza bei ya petroli, ambapo mtu wa kawaida anataabika. Hivi leo, PTI, wakiwa wapinzani, wanawasema wenzao. Ni hawa hawa PTI wanaoishutumu serikali hivi leo. Hata hivyo, nao pia wanafanya vivyo hivyo bila ya kuwa na suluhisho lolote kwa suala hili. 

Haya ni kwa sababu kiongozi yeyote awaye, wakati sisi ni sehemu ya mfumo wa sasa wa dunia wa urasilimali, hapapatikani suluhisho kwa suala la kurudisha nyuma bei za petroli. Hakuna kati ya hawa waitwao viongozi wenye ruwaza ya kuwatoa katika mashaka haya Waislamu wa Pakistan. Wote wameshikamanishwa na urasilimali na hawawezi kuona nje yake.

Urasilimali katika hali ya upotoshaji, unatilia mkazo kuwa kila rasilimali ya kiuchumi, ikiwemo rasilimali ya umma kama petroli, lazima ibinafsishwe. Ubinafsishwaji unapelekea wamiliki binafsi kunyonya faida kubwa kwa gharama ya umma, kwa kupanda sana bei ya mafuta. Hata hivyo, usawa wa kiuchumi unalazimisha utafauti katika aina za umiliki, kusambaza utajiri na kuzuia ulimbikizaji kwa wachache. Usimamizi wa umma, wakiwa ni jamii ya washirika, unawapatia aina maalum ya umiliki kwa ajili ya mali za umma, kama madini, maji, malisho na nishati. Dini ya Uislamu iliyoshushwa na Mwenyezi Mungu ndio pekee yenye hukumu za Kisharia juu ya ‘mali za umma’, zinazotumika kwa namna ya kipekee juu ya mahitaji ya watu jumla. Khalifah lazima atumie utajiri na mapato ya huduma za umma kwa mahitaji ya umma pekee, na kuzuia kubinafsisha, na kufanya gharama ziwe chini. Mtume (saw) amesema, «الْمُسْلِمُونَ شُرَكَاءُ فِي ثَلَاثٍ الْمَاءِ وَالْكَلَأِ وَالنَّارِ» “Waislamu ni washirika katika vitu vitatu, maji, malisho na moto (nishati)” (Ahmad)

Kwa hiyo suala hapa sio kuhusu nani kiongozi. Sasa ni muda wa kujadili suala halisi, nalo ni mfumo wenyewe. Mfumo uliopo tulioletewa ambao unatulazimisha kuusalimisha uchumi wetu kwa IMF. Ni mfumo ambao kutokana nao mtu wa kawaida anataabika, na kiongozi yeyote anayezungumza juu ya afueni katika mfumo huu uliopo anatoa matumaini ya uongo.

Kile ambacho lazima kitambulike hivi leo ni kwamba kuna ombwe la kisiasa nchini Pakistan, ambapo upande mmoja kuna PML-N, na upande mwengine kuna PTI, vyote viwili havina uwezo, havina ruwaza, visivyomudu kutatua masuala ya Waislamu wa Pakistan na kujidhalilisha chini ya IMF na Amerika.

Kwa kuangalia tu suala la bei ya petroli, tunagundua kuwa hakuna kati yao katika mfumo wa sasa wa kisiasa wenye suluhisho kwa tatizo hilo, na hii ipo hivyo kwa kila tatizo linalowakumba Waislamu wa Pakistan hivi leo.

Ombwe hili la kisiasa lazima lizibwe na mfumo wa kisiasa wa Uislamu, unaotupa ruwaza ya kujenga uchumi huru, kwa kutumia sera za kiuchumi za Kiislamu, na hatimaye kutabikisha mfumo wa kiulimwengu wa Kiislamu utakaopambana na mfumo wa kiulimwengu wa Kimagharibi wa kibepari, ambao kutokana nao, hivi leo Waislamu wa Pakistan wanataabika.

Wabebaji Da’wah wanaoujali Ummah watambue kuwa huu ni muda muhimu sana kwa Pakistan na kwamba vijana wa Ummah wa Kiislamu lazima wachukue hatua. Katika wakati ambapo hakuna katika wadau wa kisiasa wenye suluhisho kwa kadhia zinazoukumba Ummah wa Kiislamu, ni jukumu la Wabebaji Da’wah kuelezea masuluhisho ya Kiislamu kwa watu wa Pakistan na kwa watu wenye nguvu nchini Pakistan.

Enyi Wabebaji Da’wah, mna uwezo wa kuwa kina Mus’ab ibn Umayr (ra) wapya. Huu sio muda wa kukaa kimya. Ni muda wa kumaliza mateso ya Waislamu wa Pakistan kwa kusimamisha Khilafah kwa Njia ya Utume.

Kwenu nyinyi, Enyi watu wenye nguvu wa Pakistan, lazima mtambue kuwa kama Pakistan itaendelea kufuata maagizo ya IMF, kama inavyofanya hivi leo, tutaishia pabaya kuliko Sri Lanka. Hivi sasa ni muda wenu kuwa kama Ansar na kutoa Nussrah kwa ajili ya kuitabikisha Khilafah nchini Pakistan, ili mateso ya Ummah wa Kiislamu yaishe na bishara njema ya Mtume (saw) iweze kutimizwa. Mtume (saw) amesema, «ثُمَّ تَكُونُ خِلَافَةٌ عَلَى مِنْهَاجِ النُّبُوَّة» “…Kisha itakuwepo Khilafah kwa njia ya Utume…” (Ahmad)

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Qasim Abdullah – Wilayah Pakistan

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu