Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vichwa vya Habari 15/06/2022

Vichwa vya Habari:

• Silaha za Kiulimwengu za Nyuklia Zatarajiwa Kukua kwa Mara ya Kwanza kwa Miongo Mingi

• Ukraine Yakiri Urusi Yashinda katika Jimbo la Donbas Nakuomba Silaha Zaidi

• Urusi Yapata $100 bilioni kutokana na Mahuruji ya Kawi tangu Uvamizi wa Ukraine

• Watu nchini Pakistan Waombwa Kunywa Vikombe Vichache vya Chai

Maelezo:

Silaha za Kiulimwengu za Nyuklia Zatarajiwa Kukua kwa Mara ya Kwanza kwa Miongo Mingi

Mrundikano wa silaha za nyuklia duniani unatarajiwa kuongezeka katika miaka ijayo kwa mara ya kwanza tangu Vita Baridi kutokana na mivutano ya kimataifa, shirika kuu la uangalizi wa silaha limesema. Katika ripoti yake ya kila mwaka Utafiti wa Amani wa Kimataifa wa Stockholm (SIPRI) ulisema kuwa nchi zote tisa zenye silaha za nyuklia zinaongeza au kuboresha maghala yao. Kwa miongo kadhaa, idadi ya silaha za nyuklia kote ulimwenguni imekuwa ikipungua polepole. Sasa ni chini ya khumusi moja ya kile kilichokuwa kwenye ghala za dola za nyuklia wakati wa kilele cha Vita Baridi katika miaka ya thamanini. Mwaka jana, hata hivyo, SIPRI tayari ilikuwa imetambua mwelekeo wa kurudi nyuma wa mabadiliko kuelekea silaha za kisasa zaidi za nyuklia. "Tunasisitiza kwamba vita vya nyuklia haviwezi kushindwa na lazima kamwe visipiganwe," Marekani ilisema katika taarifa ya pamoja mwanzoni mwa Januari. Lakini SIPRI ilibainisha kuwa nchi zote tano tangu wakati huo zimepanua zaidi au kuboresha silaha zao za kisasa. Marekani inatazamia kuzifanya kuwa za kisasa silaha zake za nyuklia licha ya kushinikiza mataifa mengine kukubaliana na mikataba ya upokonywaji silaha za nyuklia na vikwazo.

Ukraine Yakiri Urusi Yashinda katika Jimbo la Donbas Nakuomba Silaha Zaidi

Katika wiki za hivi karibuni, maafisa wa Ukraine wamekuwa wazi zaidi kuhusu hasara zao kwenye uwanja wa vita huku wakiisihi Marekani na mataifa mengine ya Magharibi kutuma silaha zaidi. Maafisa wa Ukraine waliliambia gazeti la ‘The Wall Street Journal’ kwamba bila ya ongezeko kubwa la msaada wa kijeshi, Ukraine itakabiliwa na kushindwa katika jimbo la Donbas mashariki. "Katika vita hivi, ushindi utakuwa kwa upande ambao una silaha nyingi na bora zaidi. Na, ikiwa Ukraine haipati silaha za kutosha kwa wakati, itachuruzika damu,” alisema Anton Gerashchenko, mshauri wa waziri wa mambo ya ndani wa Ukraine. Maafisa wa Marekani pia wanatarajia Urusi kuendelea kupata mafanikio katika jimbo la Donbas. Afisa mmoja wa Pentagon aliliambia gazeti la ‘The Washington Post’ kwamba kuna uwezekano Urusi itadhibiti eneo lote la Luhansk ndani ya wiki chache.

Urusi Yapata $100 bilioni kutokana na Mahuruji ya Kawi tangu Uvamizi wa Ukraine

Urusi ilipata karibu $100bilioni kutokana na mahuruji ya mafuta na gesi katika siku 100 za kwanza za vita nchini Ukraine, kulingana na ripoti moja. Mapato yamekuwa yakishuka tangu Machi, kwani nchi nyingi ziliepuka usambazaji wa Urusi, lakini zinaendelea kuwa nyingi, Kituo huru cha Utafiti wa Nishati na Hewa Safi (CREA) kiligundua. Pia kilionya juu ya mianya inayoweza kutokea katika juhudi za kuzuia uagizaji kutoka Urusi. Muungano wa Ulaya, Marekani na Uingereza ni miongoni mwa zile zilizoahidi kupunguza uagizaji wa bidhaa za Urusi. Lakini ripoti ya CREA iligundua Urusi bado ilipata $97bilioni katika mapato kutokana na mauzo ya mafuta ya kisukuku katika siku 100 za kwanza za mzozo wa Ukraine, kuanzia tarehe 24 Februari hadi 3 Juni. Muungano wa Ulaya ulipata 61% ya uagizaji huu, wenye thamani ya takriban $59bilioni. Kwa ujumla, mauzo ya mafuta na gesi ya Urusi yanashuka na mapato ya Moscow yanayotokana na mauzo ya nishati pia yamepungua kutoka kilele cha zaidi ya $1bilioni kwa siku mnamo mwezi Machi. Lakini mapato bado yalizidi gharama ya vita vya Ukraine katika siku 100 za kwanza - huku CREA ikikadiria kuwa Urusi inatumia karibu $876 milioni kwa siku katika uvamizi huo. Ripoti ya CREA ilisema vikwazo vya mafuta vilivyopangwa na EU vitakuwa na athari kubwa. Lakini ilionya kiasi kikubwa cha mafuta yasiyosafishwa ya Kirusi sasa yanasafirishwa kwenda India, ambayo iliongeza sehemu yake ya jumla ya mauzo ya nje ya Urusi kutoka karibu 1% kabla ya uvamizi wa Ukraine hadi 18% mwezi Mei. Ripoti hiyo ilisema "sehemu kubwa" yake yalikuwa yakisafishwa na kuuzwa - aghlabu kwa wateja nchini Marekani na Ulaya - ambayo ilielezea kama "mwanya muhimu wa kuzibwa".

Watu nchini Pakistan Waombwa Kunywa Vikombe Vichache vya Chai

Watu nchini Pakistan wametakiwa kupunguza kiwango cha chai wanachokunywa ili kuweka uchumi wa nchi hiyo kuendelea. Kunywa vikombe vichache kwa siku kunaweza kupunguza bili za juu za uagizaji za Pakistan, waziri mkuu Ahsan Iqbal alisema. Akiba ya chini ya fedha za kigeni nchini humo - ambayo kwa sasa inatosha kwa chini ya miezi miwili kwa bidhaa zote zinazoagizwa kutoka nje - zimeiacha katika hitaji la haraka la fedha. Pakistan ndio muagizaji mkuu wa chai duniani, ikinunua zaidi ya thamani ya $600 milioni (£501 milioni) mwaka jana. "Ninatoa wito kwa taifa kupunguza unywaji wa chai kwa kikombe kimoja hadi viwili kwa sababu tunaagiza chai kwa mkopo," Bw Iqbal alisema, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Pakistan. Wafanyabiashara wanaweza pia kufunga vibanda vyao vya soko saa 20:30 ili kuokoa umeme, alipendekeza. Ombi hilo lilikuja wakati akiba ya fedha za kigeni ya Pakistan ikiendelea kushuka kwa kasi - na kuweka shinikizo kwa serikali kupunguza gharama kubwa za uagizaji na kuhifadhi fedha nchini humo. Ombi la kupunguza unywaji wa chai limeenea kwenye mitandao ya kijamii, huku wengi wakishuku matatizo makubwa ya kifedha nchini humo yanaweza kutatuliwa kwa kukata kinywaji hicho chenye madini ya kafeini.

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu