Jumamosi, 11 Shawwal 1445 | 2024/04/20
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Vichwa vya Habari: 11/01/2023

Vichwa vya Habari:

• Watawala wa Pakistan Waomba Fedha Zaidi

• Misri Yaapa Kupunguza Dori ya Ziada ya Jeshi katika Uchumi chini ya Kifurushi cha Kifedha cha Uokozi cha IMF

• Gharama za Vita vya Ukraine Zaongezeka kwa Moscow

Maelezo:

Watawala wa Pakistan Waomba Fedha Zaidi

Jumuiya ya kimataifa imeahidi zaidi ya dolari bilioni 9 kusaidia Pakistan kujijenga upya baada ya mafuriko makubwa ya kiangazi mwaka jana, yaliyoelezwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres kama "monsuni ya maafa." Ahadi hizo zilitolewa katika Kongamano la Kimataifa la Pakistan Inayostahamili mabadiliko ya tabianchi jijini Geneva, Uswisi, lililoandaliwa na waziri mkuu wa Pakistan Muhammad Shehbaz Sharif na Guterres. Sharif amesema Pakistan inahitaji kima cha chini cha dolari bilioni 16.3 katika kipindi cha miaka mitatu ijayo ili kuanza ufufuaji na ujenzi mpya, ambao nusu yake itafikiwa na rasilimali za ndani. Ahadi kubwa zaidi - dolari bilioni 4.2 - ilitoka kwa Kundi la Benki ya Maendeleo ya Kiislamu. Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia kwa Asia Kusini, Martin Raiser, alitangaza mchango wa dolari bilioni 2. Pakistan inatarajiwa kulipa hadi dolari bilioni 23 mwaka 2023 ikijumuisha mashirika ya kimataifa kama vile IMF na Benki ya Dunia. Mtu angeweza kufikiria kufutwa kwa deni hili ingekuwa ndio mahali pa kuanzia kwa watawala wa Pakistan badala ya kuomba pesa zaidi.

Misri Yaapa Kupunguza Dori ya Ziada ya Jeshi katika Uchumi chini ya Kifurushi cha Kifedha cha Uokozi cha IMF

Misri imejitolea kupunguza dori ya jeshi katika uchumi kama sehemu ya kifurushi chake cha uokozi cha IMF cha $3 bilioni, wakati nchi hiyo ya Kiarabu inakabiliana na mgogoro wa fedha za kigeni, pauni inayodhoofika na kupanda kwa mfumko wa bei. IMF ilisema katika taarifa yake kwamba mageuzi "muhimu" ya kimuundo ambayo Cairo ilikubali ni pamoja na "kusawazisha uwanja kati ya sekta ya umma na ya kibinafsi" kama sehemu ya sera ya umiliki wa serikali iliyoidhinishwa na Rais Abdel Fattah al-Sisi. Mfuko huo ulisema sera hiyo itashughulikia mashirika yote ya serikali, ikiwemo "kampuni zinazomilikiwa na jeshi", katika hali ya nadra ya kukiri kwa IMF jinsi jeshi lilivyopanua nyayo zake katika uchumi wa Misri tangu mkuu wa zamani wa jeshi kunyakua mamlaka katika mapinduzi ya 2013. Wanauchumi na wafanyibiashara wa Misri wamelalamika kwa muda mrefu kwamba dori ya jeshi katika uchumi ilijaza sekta ya kibinafsi na kuwatisha wawekezaji wa kigeni. Jeshi, taasisi yenye nguvu zaidi nchini, limeepushwa na kutozwa baadhi ya kodi na biashara zake zimefichika sana. Cairo ililazimika kwenda kwa IMF mwaka jana baada ya wawekezaji wa kigeni kuondoa takriban dolari bilioni 20 kutoka kwa soko la madeni la Misri kipindi cha uvamizi wa Urusi nchini Ukraine. Utiririkaji wa mtaji nje ulichochea mgogoro wa fedha za kigeni na kulazimisha Cairo kugeukia mataifa ya Ghuba kwa ajili ya uokoaji wa mabilioni ya dolari. Wafanyibiashara wanatumai ukubwa wa mgogoro uliopo sasa utalazimisha mamlaka kuchukua hatua. Lakini utawala wa Sisi hapo awali uliahidi kupunguza dori ya jeshi katika uchumi na kubinafsisha makampuni yanayomilikiwa na jeshi, lakini maendeleo kidogo tu yalipatikana.

Gharama za Vita vya Ukraine Zaongezeka kwa Moscow

Katika hali isiyo ya kawaida, waziri wa fedha wa Urusi amekiri kudorora kwa hali ya fedha za umma ya Urusi. Vita vya Ukraine vinaigharimu Urusi zaidi kuliko ilivyo zalisha kutokana na mapato ya rekodi ya mafuta na gesi, huku pengo la bajeti ya nchi hiyo likiongezeka kwa kiasi kikubwa mwaka wa 2022. Nakisi ya umma kwa mwaka jana ilikuwa $48 bilioni, kulingana na Waziri wa Fedha Anton Siluanov. Kabla ya Urusi kuivamia Ukraine mwezi Februari mwaka jana, Moscow ilikuwa imetabiri ziada ya bajeti. Lakini uidhinishaji huu rasmi wa kuzorota kwa fedha za umma unajiri licha ya rekodi ya mapato ya mafuta na gesi kama matokeo ya bei ya juu ya nishati na uwezo wa Moscow wa kuelekeza mauzo yake ya mafuta kwenda Asia. Moscow ilishughulikia nakisi hiyo kwa kuelekeza pesa kutoka kwa hazina ya utajiri huru ya Urusi, ukopaji wa serikali na ushuru wa mara moja kwa Gazprom, ukiritimba wa gesi ya serikali. Inaweza kuonekana kuwa vikwazo vya Magharibi vinaikumba Urusi huku vita vya Ukraine vikiendelea, wakati Urusi imeongeza mapato yake kutoka kwa nishati na malighafi, kiasi cha mauzo ya nje kimeshuka, ambayo ina maana kwamba Urusi inauza nje kidogo na hii itakuwa na athari kubwa kwa uchumi wa Urusi wakati vita vinaendelea. Sasa tunaona hili huku waziri wa fedha wa Urusi akikiri kuongezeka kwa nakisi ya bajeti ya taifa hilo.

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu