Alhamisi, 18 Ramadan 1445 | 2024/03/28
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Porojo za Vita Dhidi ya Ugaidi Zinaendelea

(Imetafsiriwa)

Habari:

Mnamo Jumatatu tarehe 19/09/2022 Tanzania iliungana na nchi nyingine za Afrika katika kutekeleza Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Afrika (AU) wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi. Baada ya kupitishwa azimio la kuridhiwa kwa itifaki hiyo, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Yusuph Masauni alisema kuwa Tanzania ina nafasi kubwa ya kupata manufaa kadhaa, ikiwa ni pamoja na kuimarisha ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao na kurahisisha ubadilishanaji wa taarifa za kiintelijensia kuhusu ugaidi kupitia ushirikiano wa karibu kutoka kwa nchi wanachama.

Maoni:

Ni ukweli ulio wazi kwamba propaganda ya ‘vita dhidi ya ugaidi’ nchini Tanzania, mataifa ya Afrika na nchi zinazoendelea kwa ujumla ni mbinu ya kikoloni ya Wamagharibi ya kupambana na Uislamu, unyonyaji na uingiliaji wa mifumo ya usalama. Wakoloni Wamagharibi wanalazimisha mataifa dhaifu  kuwaua, kuwatesa na kuwafunga watu wao wenyewe kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi kwa kubadilishana na hongo ya nchi za Magharibi inayoitwa fedha kwa ajili ya kupambana na ugaidi.

Nchini Tanzania haijawahi kutokea kesi ya wazi ya “gaidi” yeyote aliyekamatwa, licha ya propaganda za muda mrefu. Juni, 2019 aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Bwana Kangi Lugola alithibitisha kuwa hakuna tishio la ugaidi nchini Tanzania, kabla ya hapo Februari 2017 aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Harrison Mwakyembe aliliambia bunge kuwa hakuna taarifa yoyote ya tishio la ugaidi iliyoripotiwa nchini katika miaka ya hivi karibuni.

Taarifa zote hizi rasmi zinathibitisha ukweli mmoja, ambao ni kutokuwepo ugaidi wa kweli nchini badala yake kuna matumizi ya propaganda ya kimataifa ya vita dhidi ya ugaidi inayolenga Uislamu na Waislamu duniani kote na pia kuvuruga amani na maelewano na kurahisisha njia ya unyonyaji wa Wamagharibi kwa rasilimali za ulimwengu wa tatu.

Vyombo vya kusimamia sheria nchini Tanzania kwa muda mrefu vimekuwa vikitumia suala la ugaidi kutengeneza na kubambikia kesi dhidi ya Waislamu, wanaharakati na viongozi wao.  Kesi hizi za kubambikiwa zimekuwa zikiisha kwa aibu ambapo jamhuri siku zote hushindwa kuleta ushahidi wowote kuthibitisha madai yao.

Zaidi ya hayo, kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi na visingizio vingine, wengi wameteseka mikononi mwa vyombo vya sheria ambavyo vimekuwa vikiwaua, kuwapora, kuwateka nyara, kuwaweka kizuizini kwa muda mrefu bila kufunguliwa mashtaka nk.

Kwa mfano, mwaka wa 2006, maafisa waandamizi wa jeshi la Polisi akiwemo SSP Christopher Bageni, waliwaua wafanyibiashara watatu wa madini na dereva wa teksi. Pia zaidi ya wahanga 380 hawajulikani waliko hadi leo kufuatia uvamizi wa serikali katika vijiji vya Mkuranga, Kibiti na Rufiji mwaka 2017, uvamizi ambao “haukufanyika kwa mujibu wa sheria na ulioambatana na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na mateso na mauaji ya kiholela” (The East African, Mei 05, 2018)

Bila ya kusahau kwamba mamia kama sio maelfu ya Waislamu na wengine waliwekwa kizuizini kwa miaka mingi bila kesi zao kusukilizwa, kama vile viongozi wa kikundi cha Uamsho kutoka Zanzibar waliowekwa kizuizini kwa takriban miaka minane na kufunguliwa mashtaka ya kubambikiwa yanayohusiana na ugaidi.  Kisha serikali iliyabwaga mashtaka yao kwa aibu mwaka 2021. Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Sylvester Mwakitalu, alithibitisha kwa waandishi wa habari kufutwa kwa mashtaka yote. Hali kama hiyo iliwakuta wanachama watatu wa Hizb ut Tahrir Tanzania ambao walizuiliwa bila kesi yao kusikilizwa kwa zaidi ya miaka minne baada ya kushtakiwa kwa kesi ya kubambikiwa ya ugaidi, ambapo hatimaye waliachiliwa huru tarehe 22 Februari 2022, kufuatia DPP kuthibitisha kwamba hawana ushahidi wa kukinaisha kuendelea na mashtaka yanayodaiwa.

Pia, Mwenyekiti wa chama kikuu cha siasa cha upinzani (Chadema) nchini Tanzania, bwana Freeman Mbowe alikamatwa Julai 2021 katika uvamizi wa usiku jijini Mwanza, kabla ya mkutano wa hadhara wa kudai marekebisho ya katiba na kufunguliwa mashtaka yanayohusiana na ugaidi, kisha aliachiwa huru baada ya kukaa rumande kwa miezi saba.

Hiyo ni mifano michache tu kati ya mamia na maelfu ya watu waliowekwa kizuizini kwa kesi za kubambikiwa zinazohusiana na ugaidi ambapo 99.9% ni Waislamu ambao serikali imeshindwa kuthibitisha madai yao mbele ya mahakama hata baada ya miaka mingi ya kile kinachoitwa upelelezi. Hii ina maana kwamba hakuna hata mmoja wao aliyefanya vitendo vyovyote vya ugaidi, ndiyo maana jamhuri ilishindwa kuwasilisha ushahidi wowote thabiti dhidi yao.  

Tunasisitiza tena kwamba, kampeni ya kupambana na ugaidi ni ajenda ya kigeni ya Kimagharibi na lazima ikomeshwe, kwa kuwa sheria na mikataba yake ni chombo cha kikatili cha kupambana hususan na Waislamu na Uislamu.

Imeandikwa kwa ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Said Bitomwa

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu