Ijumaa, 19 Ramadan 1445 | 2024/03/29
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

Afisi ya Habari
Wilayah Jordan

H.  21 Sha'aban 1443 Na: 1443 / 17
M.  Alhamisi, 24 Machi 2022

 Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Sheria Mpya ya Vyama ya Jordan Haizalishi Vyama vya Kisiasa kwa ajili ya Umma... Bali, Vyama kwa ajili ya Serikali

 (Imetafsiriwa)

Mnamo Jumatatu, 21/3/2022, Baraza la Wawakilishi liliidhinisha rasimu ya sheria ya vyama vya kisiasa kama ilivyorekebishwa na Seneti, baada ya kuidhinishwa hapo awali na Baraza la Wawakilishi mnamo tarehe 8/3/2022, baada ya kuidhinisha vifungu vyake 43, katika vikao vinavyoendelea kwa muda wa siku tatu.

Sababu za rasimu ya sheria hiyo ya vyama iliyopendekezwa hapo awali na Kamati ya Kifalme ya Uboreshaji Mfumo wa Kisiasa, chini ya jina la mageuzi ya kisiasa, zitajwa kama: "Kwa kuzingatia imani ya dori inayochezwa na vyama katika maisha ya kisiasa ya Jordan, kama idara ya juu zaidi ya shirika katika jamii yoyote kueleza misimamo na maslahi, na katika harakati za kufikia matarajio ya watu wa Jordan, na matarajio yao ya maisha bora, sheria mpya ya vyama vya siasa ilikuja kwa sababu zifuatazo: kuwezesha vyama kufikia uundaji wa serikali za kibunge zilizoegemea upande mmoja, au kushiriki katika vyama hivyo, kuunda vyama vya kisiasa vyenye utaratibu, viongozi wenye sifa stahiki za kisiasa, hasa vijana, wenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za kisiasa, kiuchumi na kijamii, na kuwezesha vyama kushiriki katika chaguzi mbalimbali na kuvisaidia kuhusika na masuala ya umma.”

Miongoni mwa vifungu muhimu zaidi vya rasimu hii ya sheria kuhusu vyama ni ufafanuzi wa “chama” kama “shirika la kisiasa la kitaifa linalojumuisha watu wa Jordan ambao wameunganishwa na maadili ya uraia, malengo, mipango, ruwaza na mawazo ya pamoja, na yenye lengo la kushiriki katika maisha ya kisiasa na kazi za umma kwa njia za amani, za kidemokrasia kwa madhumuni halali na kwa kushiriki katika aina zote za chaguzi, zikiwemo chaguzi za wabunge na kuunda au kushiriki katika serikali,” na iliidhinisha “haki ya kuanzisha vyama na kushiriki katika chaguzi hizo,” na ilibainisha "kuzuia madhara ya moja kwa moja au yasiyo ya moja kwa moja kwa Mjordan yeyote, ikiwa ni pamoja na kukiuka haki zake za kikatiba au kisheria, au kuwajibishwa." Sheria hii pia ilikubaliana juu ya "kanuni za kuanzisha vyama, kwa kuzingatia uraia na usawa kati ya Wajordan, kujitolea kwa demokrasia, na kuheshimu vyama vingi vya kisiasa, na kukataza kuanzisha chama kwa misingi ya kidini, madhehebu, kikabila au makundi." Rasimu ya sheria hiyo iliweka vikwazo na masharti ya kina ya uundaji na utendakazi wa vyama, ambayo yalihitaji vifungu 42 vya kina, kana kwamba ni katiba ya nchi. Haikuacha chochote, hakuna mwanya au kizuizi, ili vyama vitakavyoundwa au kurekebisha hali yao visiondoke kwenye utiifu au dira ya mfumo katika utawala. Mbali na ubovu wa misingi na sababu za mradi huu, kwani muundo wa kisiasa nchini Jordan unazunguka mfumo tawala na bunge halina mamlaka makubwa. Serikali hizo huteuliwa na mfalme, na hata serikali zijazo za bunge ziliondolewa mamlaka yake kwa kubadilishana na kupanua mamlaka ya mfalme, na kuweka mipaka ya maono yake ya kisiasa kwa Baraza la Usalama la Kitaifa. Hayo yote hayana umuhimu hata katika muktadha wa demokrasia mbovu ya kisekula ambayo inadai kuisimamia na ambayo rasimu ya sheria ya chama imejikita.

Ama kuhusu uhalali wa kuunda, kuendesha na kutoa leseni kwa vyama vya kisiasa, tunaangazia yafuatayo:

1- Umma wa Kiislamu unaishi katika hali ya kipekee bila ya kuwepo dola inayojumuisha yote yenye msingi wa imani ya Kiislamu, ambayo ni Dola ya Khilafah kama ilivyo sasa. Itatabikisha hukmu zote za Shariah ndani na nje. Kwa vile siasa ni kuchunga na kujali mambo ya umma, chama cha kisiasa katika Uislamu ni kundi la waumini lililokusanyika kwa misingi ya Uislamu, ambao ni kheri yote, na kuulingania kama itikadi ya kisiasa na mfumo unaotawala maisha. Kitendo cha kisiasa cha kuregea kwa Uislamu katika maisha ni miongoni mwa matendo makubwa kabisa ya kuamrisha mema na kukataza maovu na kulingania kheri, jambo ambalo limekuja katika Aya tukufu, Mwenyezi Mungu (swt) asema:

[وَلْتَكُنْ مِنْكُمْ أُمَّةٌ يَدْعُونَ إِلَى الْخَيْرِ وَيَأْمُرُونَ بِالْمَعْرُوفِ وَيَنْهَوْنَ عَنِ الْمُنْكَرِ وَأُولَئِكَ هُمُ الْمُفْلِحُونَ]

“Na uwe kutokana na nyinyi umma unao lingania kheri na unao amrisha mema na unakataza maovu. Na hao ndio walio fanikiwa.” [Aal-i-Imran: 104].

2- Kwa kuregelea Aya tukufu iliyotangulia, Rasimu ya Katiba ya Dola ya Khilafah iliyotayarishwa na Hizb ut Tahrir, inayotokana na Quran na Sunna kuhusu vyama vya kisiasa, imesema yafuatayo: “Waislamu wana haki ya kuanzisha vyama vya kisiasa kuwahisabu watawala, au kufikia madaraka kupitia Ummah, kwa sharti kwamba msingi wake ni itikadi ya Kiislamu, na kwamba hukmu wanazozitabanni ni hukmu za Kiislamu. Kuanzishwa kwa chama hakuhitaji leseni yoyote, na kundi lolote ambalo msingi wake ni kitu chochote kisichokuwa Uislamu limepigwa marufuku."

3- Haijuzu kwa kundi miongoni mwa Waislamu kujengwa juu ya kitu chochote kisichokuwa msingi wa kama imani na mfumo. Uanzishwaji wa vyama kwa misingi ya kidemokrasia, ya kisekula inayotenganisha Dini na maisha, kama ilivyoelezwa katika rasimu ya sheria ya Jordan kuhusu vyama inapingana na Shariah, kama ambavyo hairuhusiwi kwa vyama kuwa na misingi ya kitaifa, kizalendo, ambayo inaendeleza mgawanyo wa ukoloni wa umoja wa Umma wa Kiislamu. Mwenyezi Mungu (swt) asema:

 [إِنَّ هَذِهِ أُمَّتُكُمْ أُمَّةً وَاحِدَةً وَأَنَا رَبُّكُمْ فَاعْبُدُونِ] 

“Kwa hakika huu umma wenu ni umma mmoja, na Mimi ni Mola wenu Mlezi. Kwa hivyo niabuduni Mimi” [Al-Anbiya: 92]. 

4- Kazi ya kifikra na kisiasa ya chama cha kisiasa imejikita katika kuchunga mambo ya Ummah mzima katika Uislamu, kwa umakini wake wa kuwa kwa mujibu wa yale yaliyoelezwa katika Qur’an na Sunnah. Kinajumuisha maeneo yote ya maisha na hakuna mtu aliyeachwa nyuma. Vyama vya kisiasa katika Umma wa Kiislamu, katika hali ambapo dola ipo, ni walinzi wa jamii. Ndivyo vinavyofanya kazi miongoni mwa watu kuzuia kuanguka kwake, na pia vinawahisabu watawala juu ya uchungaji kwa misingi ya Uislamu na kwa kiwango kamili. Na ikiwa dola ya Khilafah haipo katika Ummah, lengo lao ni kuisimamisha.

5- Haijuzu kwa vyama vya kisiasa kushiriki katika utawala wa kisekula unaoutenganisha Uislamu madarakani, si kwa kuunda serikali wala kwa kushiriki ndani yake. Mwenyezi Mungu (swt) asema:

 [وَمَن لَّمْ يَحْكُم بِمَا أَنزَلَ اللَّهُ فَأُولَٰئِكَ هُمُ الْفَاسِقُونَ]

“Na wasio hukumu kwa yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu basi hao ndio wapotofu” [Al-Ma’ida: 47].

Na vyama vya kisiasa vinavyoamini Ummah wao haviruhusiwi kunyamaza kimya kuhusu utawala unaofanya mapatano na maadui zake, unaopora mali yake na kukiuka mamlaka yake kwa kuweka kambi za kijeshi katika ardhi zake, na kuuweka rehani uchumi wake kwa dola haribifu za kikoloni.

6- Vyama vya kisiasa ndio wahusika na vishawishi katika kubadilisha mfumo wa utawala na sio watu wake. Serikali ni chombo cha utendaji kwa vipimo, ukinaifu na mifumo ya Ummah, na Ummah ni chombo kisicho na shughuli. Chama cha kisiasa cha kimfumo ni chama kinachofanya kazi katika Ummah kubadilisha fahamu, vipimo na ukinaifu wake, na kisha kuregesha mamlaka yake yaliyonyakuliwa ya kusimamisha dola na kuchagua mtawala kulingana na mfumo wake.

7- Na chama cha kisiasa ambacho Uislamu umekiweka kuwa ni wajibu wa kujitosheleza (fardh kifaya), ikiwa kinataka kufikia “matarajio ya watu wa Jordan na matarajio yao ya maisha bora,” kama ilivyoelezwa katika sababu za sheria hii mpya. lazima kiwe chama cha Ummah na sio serikali inayotawala, maana yake ni kwamba dori yake sio tu kufuatilia na kusahihisha makosa yakitokea, bali ni pamoja na kila aina ya bidii, uwajibikaji, usimamizi na uchungaji kwa ufahamu na ushauri, kwa njia ambayo inahakikisha maendeleo na maboresho endelevu katika fikra na hisia, na kudhamini nafasi ya Waislamu, na vilevile kudhamini ubwana wao wa kifikra, kisiasa, kiuchumi na kihadhara. Kinataka pamoja na Ummah wake kufikia matamanio yake kuelekea mradi wake wa mwamko kwa kuregea Dola ya Khilafah, na sio kama msaada kwa serikali katika kuendeleza utiifu wake kwa mkoloni kafiri wa Magharibi, na miradi yake ya pamoja ya kulipa nguvu umbile la Kiyahudi, ili kwamba sifa ya chama cha siasa chenye kufikia matarajio ya Ummah wake inalingana nacho.

Hizb ut Tahrir, ambayo ilianzishwa kwa kuitikia amri ya Mwenyezi Mungu, kwamba angalau kundi moja lazima liasisiwe, kama inavyoonyeshwa na Aya tukufu, imetoa mfano kama muundo wa chama cha kimfumo kwa mapambano yake ya kifikra, kazi ya kisiasa, ulinganizi wake kwa Uislamu na kutabanni maslahi ya Ummah wake. Ni chama kilichojengwa juu ya msingi wa fikra na hisia za jamii, ni chama cha kwanza kabisa cha kisiasa. Ulinganizi wake ukawa wa watu wote, kumlingania yeyote aliye na nia ya dhati ya kuunda chama cha kisiasa kuiga mfano wake katika fikra, njia na malengo yake. Kazi yake imenakiliwa katika machapisho yake, juu ya orodha ni At-Takatul Al-Hizbi (Muundo wa Chama).

 [وَأَنَّ هَٰذَا صِرَاطِي مُسْتَقِيماً فَاتَّبِعُوهُ وَلَا تَتَّبِعُوا السُّبُلَ فَتَفَرَّقَ بِكُمْ عَن سَبِيلِهِ]

“Na kwa hakika hii ndiyo Njia yangu Iliyo Nyooka. Basi ifuateni, wala msifuate njia nyingine, zikakutengeni na Njia yake.” [Al-An’am: 153].

Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir katika Wilayah Jordan

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Wilayah Jordan
Address & Website
Tel: 
http://www.hizb-jordan.org/
E-Mail: info@hizb-jordan.org

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu