Alhamisi, 18 Ramadan 1445 | 2024/03/28
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Watoto wa Yemen Wanaendelea Kutolewa Kafara katika Vita kati ya Uingereza na Amerika Vilivyoikumba Nchi Hiyo

Habari:

Umoja wa Mataifa umeripoti kwamba mashambulizi ya anga mnamo Alhamisi 6 Agosti yaliyofanywa na muungano wa Saudia na Imarati katika jimbo linaloshikiliwa na Houthi la al-Jawf kaskazini mwa Yemen yamewauwa kwa uchache watoto 9. Wizara ya Afya katika maeneo yanayo dhibitiwa na Houthi pia ilieleza kuwa sambamba na vifo hivyo, watoto na wanawake 12 walijeruhiwa. Hili ni shambulizi la tatu la muungano huo kwa mwezi huu mmoja uliopita ambalo lilikuwa na vifo vingi vya watoto nchini humo. Mnamo Julai 14, Umoja wa Mataifa uliripoti kuwa shambulizi la anga katika mkoa wa Hajjah liliwauwa watoto 7, baadhi yao wakiwa wenye umri wa miaka 2, huku siku iliyofuatia, wafanyikazi wa misaada waliripoti kuwa shambulizi la anga lililofanywa na muungano wa Saudia na Imarati lililoshambulia sherehe ya kupashwa tohara mtoto moja mchanga katika jimbo la Jawf liliuwa kwa uchache raia 10, wakiwemo watoto 6 na wanawake 2.

Maoni:

Kiwango cha watoto waliouwawa katika vita hivi vya wakala vya kikatili kati ya Amerika na Uingereza kwa ajili ya ushawishi wa kisiasa nchini Yemen kimefikia takriban 3500 kwa mujibu wa tarakimu za Umoja wa Mataifa. Hii haijumuishi idadi isiyo hesabika ya waliojeruhiwa kutokana na mzozo huu au ambao wamekufa kutokana na njaa, cholera na sababu zengine zilizoweza kuzuiwa kutokana na vita hivi vya miaka mitano ambavyo vimesababisha janga baya zaidi la kibinadamu ulimwenguni ambapo watoto wamekuwa waathiriwa wakuu, na ambapo asilimia 80 ya nchi sasa inahitaji msaada wa kibinadamu. Inaripotiwa kuwa mtoto chini ya umri wa miaka 5 nchini Yemen hufariki kila dakika 10 kutokana na sababu zinazoweza kuzuiwa. Mnamo Juni mwaka huu, UNICEF ilieleza kuwa watoto milioni 2.4 nchi humo wako ukingoni mwa baa la njaa na kwamba watoto milioni 9.58 hawakuweza kupata maji salama, na usafi, ikiwaweka katika hatari kubwa zaidi ya kifo kutokana na maambukizi.

Dola za kikoloni za Kimagharibi zinauchezea ulimwengu kama vile chesi, wakivizungusha vipande vyake, na kuchochea vita baina ya vibaraka wao kwa ajili ya mapato ya kisiasa na kifedha, bila ya kuzingatia gharama za kibinadamu, ikiakisi umbile la kutojali la sera ya kigeni ya kikoloni ya kirasilimali ya dola za Kimagharibi. Kwa wanaouchunguza mzozo huu zaidi ya muonekano wa juu juu, ni wazi kuwa ni zaidi ya vita vya wakala vya kimadhehebu kati ya Saudi Arabia na dola nyengine za Ghuba na Iran. Vimesukumwa na hamu ya Amerika kupata ngome ya kisiasa ndani ya nchi ambayo imekuweko katika mikono ya utawala wa kikoloni na ushawishi wa Kiingereza kwa miaka 170, ikiwemo chini ya dikteta aliye saidiwa na Uingereza Ali Abdullah Saleh. Ili kupata lengo lao, Waamerika waliwaunga mkono vibaraka wao miongoni mwa viongozi wa Houthi ili kupata mamlaka juu ya serikali ya Abdrabbuh Mansur Hadi ilio saidiwa na Uingereza jijini Sanaa. Waliitumia serikali kibaraka wao ya Saudia kuiangamiza nchi hii, kuangamiza shule na hospitali, na kuuwa maelfu ya raia wasio na hatia katika "Operesheni ya Dhoruba Kali" ili kusababisha uungaji mkono wa ummah na uhalali wa utawala wa Houthi miongoni mwa watu wa Yemen kwa kuwawasilisha kama mashujaa na watetezi wa ardhi yao dhidi ya uvamizi wa kigeni. Yote haya ilikuwa ni kuunda upya uwanja wa kisiasa wa Yemen kwa manufaa ya Amerika kupitia kuwapa vibaraka wake kipande kikubwa zaidi katika utawala wa mustakbali cha ardhi hii ya kistratejia na iliyojaa rasilimali. Wakati huo huo, Waingereza walikitumia kikaragosi chao cha eneo, Imarati kubakisha ushawishi wake nchi humu, kupitia kutangaza vita vya kikweli dhidi ya Houthi, na kujaribu kung'oa ushawishi wa Amerika Yemen Kusini, kupitia kutoa usaidizi wake kuliweka mamlakani Baraza la Mpito la Kusini linalosaidiwa na Imarati mjini Aden.

Hivyo hapa ndipo tulipofika, katika vita vya wakala vya kikoloni vinavyo sukumwa na ulafi uliopitiliza wa serikali za kikoloni za kimagharibi, na ambapo vifo vya maelefu ya watoto wa Yemen vinatazamwa kama uharibifu wa dhamana unaokubalika na gharama inayostahiki kulipwa kwa ajili ya mapato yao ya kisiasa. Hizi ni serikali ambazo hazitafuti tu kuhifadhi manufaa ya kisiasa pekee kutokana na umwagaji damu za Waislamu bali zimetengeza mamilioni kutokana na biashara ya silaha kwa pande zinazopigana. Na sisi ndio hawa hapa ndani ya mzozo ambao serikali za Waislamu na vuguvugu la Houthi wanakubali kutumiwa kama vibaraka kuwapiga vita ndugu zao Waislamu kuhudumia maslahi ya Uingereza na Amerika, licha ya kuwa Mwenyezi Mungu (swt) anasema:

(وَمَن يَقْتُلْ مُؤْمِنًا مُّتَعَمِّدًا فَجَزَآؤُهُ جَهَنَّمُ خَالِدًا فِيهَا وَغَضِبَ اللّهُ عَلَيْهِ وَلَعَنَهُ وَأَعَدَّ لَهُ عَذَابًا عَظِيمًا)

“Na mwenye kumuuwa Muumini kwa kukusudia, basi malipo yake ni Jahannamu humo atadumu, na Mwenyezi Mungu amemkasirikia, na amemlaani, na amemuandalia adhabu kubwa.” [Al-Nisaa: 93], na Mtume (saw) amesema,

«كُلُّ الْمُسْلِمِ عَلَى الْمُسْلِمِ حَرَامٌ دَمُهُ وَمَالُهُ وَعِرْضُهُ»

“Kila Muislamu kwa Muislamu mwengine, ni haramu damu yake, mali yake, na heshima yake.” Ni mzozo ambao lile linaloitwa suluhisho lililofanyiwa udalali na Umoja wa Mataifa kamwe haliwezi kuondoa maonevu na mateso ya Waislamu wa Yemen, kwani Umoja wa Mataifa mara kwa mara umethibitisha kwamba uko mbali na kuwa mwamuzi asiye egemea upande wowote katika vita, bali daima umetumika kama chombo cha sera ya kigeni ya Amerika ili kulinda maslahi ya Amerika kiulimwengu. Tunaona kwa mfano, namna gani mwezi uliopita tu, Umoja wa Mataifa ulivyo uondoa muungano unaoongozwa na Saudia kutoka katika orodha nyeusi ya dola ambazo zimeuwa na kudhuru watoto katika mzozo. Hii ni licha ya kuwa kwa mujibu wa ripoti yake wenyewe, operesheni za muungano ziliuwa au kujeruhi watoto 222 nchini Yemen mnamo 2019 pekee, na maelfu zaidi wakati wa vita hivi.

Na hivyo umwagaji damu ya watoto wa Yemen utaendelea hadi mkono wa ukoloni ukatwe kutoka katika ardhi hii, na hadi serikali, harakati na viongozi eneo hili wanaotumikia maslahi ya dola za kikoloni wang'olewe na kubadilishwa na nidhamu na uongozi huru ambao unatumikia kikweli maslahi na kulinda haki za wote walio chini ya utawala wake – Sunni au Shia kadhalika – pamoja na kutoa masuluhisho ya matatizo yote ya wanadamu. Je, nidhamu kama hii yaweza kuibuka kutoka katika chimbuko jengine mbali na Mola wa Walimwengu, Mwenyezi Mungu (swt)? Hivyo basi tunawalingania Waislamu wa Yemen kutazama mbele zaidi ya michezo ya kisiasa ya kikoloni inayoichana ardhi yao na kuifanya kuwa makaburi ya watoto wao. Tunawalingania kutoa nusra yenu ili kusimamisha kwa haraka Khilafah kwa njia ya Utume ambayo pekee inaweza kumaliza jinamizi lenu.

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Dkt. Nazreen Nawaz

Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu