Logo
Chapisha ukurasa huu

Afisi ya Habari
Afisi Kuu ya Habari

H.  20 Sha'aban 1443 Na: 1443 H / 027
M.  Jumatano, 23 Machi 2022

 Taarifa kwa Vyombo vya Habari       

Kadhia ya Hijab nchini India kutoka kwa Mtazamo wa Kiislamu

(Imetafsiriwa)

Mnamo tarehe 15 Machi 2022, Mahakama Kuu ya Shirikisho ya jimbo la India la Karnataka ilitoa uamuzi, kwamba maagizo ya sare za shule ya mamlaka za vyuo (ambazo hazikuruhusu uvaaji wa Hijab/Khimar), hazikiuki uhuru wa kibinafsi au dini, ikikataa rufaa zote zilizowasilishwa na wanafunzi 9 wa kike wa Kiislamu wanaosoma katika Vyuo Vikuu vya Serikali za kutaka wavae Hijab na Khimar. Baraza la mahakama lenye wanachama 3 lilitaja zaidi kwamba Hijab haiwezi kuchukuliwa kama sehemu muhimu ya Uislamu, na hata kunukuu vifungu vya Quran ili kuwasilisha hukumu ya mahakama. Walalamishi tisa wameamua kupeleka kesi yao katika Mahakama ya Upeo ya taifa.

Uamuzi wa Mahakama Kuu unaotumia kurasa 129 umepata sifa mbaya kwa sababu mbalimbali. Uamuzi huo ulionyesha jaribio la Mahakama Kuu ya Karnataka inayoongozwa na serikali ya BJP kufafanua mipaka ya dini kwa wafuasi wake. Inaonekana kama utabikishaji mbaya wa mtihani wa umuhimu uliofafanuliwa na mahakama ya upeo ya nchi, ambapo ilitumia kwa mara ya kwanza mnamo 1954 kufafanua mahali ambapo sheria ya serikali itaupiku msimamo wa kidini. Ilikuwa tofauti kabisa na uamuzi mwingine wa Mahakama Kuu ya Shirikisho katika jimbo jirani la Kerala (pamoja na utawala wa jimbo lisilo la BJP), ambapo ilitoa uamuzi mwaka 2016 kuhusu kesi tofauti kwamba Hijab ni sehemu muhimu ya Uislamu. Inaonekana kama hatua nyingine kubwa ya chama tawala cha BJP kuwaridhisha Mabaniani wenye msimamo mkali na kuna uwezekano mkubwa wa kuenezwa katika taasisi na majimbo mengine ya India katika siku zijazo. Ulishuhudia sherehe za kitaifa za wafuasi wa itikadi kali wa Kibaniani, wakiwemo viongozi wa BJP, ambao msimamo wao ulikuwa chuki ya wazi kwa Hijab katika Uislamu kiasi cha kuwakatisha tamaa Waislamu nchini India na duniani, wanaotaka kutekeleza uvaaji wa Hijab katika Uislamu kama faradhi.

Lakini hukmu hii isiwashangaze Waislamu nchini India na duniani kote. Ni moja ya mizunguko ya mzozo wa kiulimwengu kati ya Uislamu na Ukafiri. Dhihirisho la mzozo huu sio tu katika mataifa 'yanayoonyesha' aina tofauti za Demokrasia, lakini pia katika ulimwengu wa Kiislamu ambao una aina zake tofauti za demokrasia, ikiwa sio udikteta. Tutaangalia mitazamo michache juu ya jambo hili ambalo ni muhimu sana kwa kila Muislamu.

1. Hijab na Khimar ni faradhi kwa Waumini wanawake (baada ya kubaleghe), iliyothibiti katika Quran na Sunnah, hivyo kukosa kushikamana nayo ni kuasi amri ya Mwenyezi Mungu (swt). Ni lazima itetewe kama amri ya Mwenyezi Mungu (swt) kwa wanawake, na kwa hakika ni utetezi sahihi. Mwelekeo wa kuitetea kama ‘dhihirisho la uhuru’ ni mbaya na ni lazima uepukwe, licha ya nia na matokeo yanayokusudiwa. Waislamu wanapaswa kutambua kwamba kutekeleza faradhi hii hakuathiriwi na uamuzi wowote wa mahakama kwani hakika haina hadhi mbele ya Mwenyezi Mungu (swt); badala yake, Waislamu lazima wajifunge kikamilifu faradhi hii.

2. Waislamu wanapaswa kutambua madai ya uongo ya nchi za Kidemokrasia za ulimwengu. Demokrasia kwa mujibu wa ‘Usekula’ inadai kulinda dini. Hata hivyo, maadili yanayodaiwa kuwa ya kisekula yanagongana kwa nguvu sana na matakwa ya kutabikisha Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt) katika maisha ya umma kama vile kuharamisha pombe, kamari, zina, Riba na mengineyo - hata kama matakwa hayo yapo katika ardhi za Kiislamu. Demokrasia inataka kwamba maagizo na marufuku ya sheria kwa watu, yaamuliwe katika chombo cha utunzi wa sheria kilichochaguliwa bila kujali amri ya Mwenyezi Mungu (swt). Watu wa ardhi zisizokuwa za Kiislamu wanaendelea kupoteza imani na Demokrasia kwa unyanyasaji na ufisadi uliokithiri wanaoushuhudia na mmomonyoko wa haki na riziki zao. Waislamu wanapaswa kutambua kwamba utabikishaji wa Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt) pamoja na hisia ya juu ya uwajibikaji na ikhlasi utaleta amani na ustawi wa dunia.

3. Waislamu wanapaswa kutambua kwamba nchi za Kidemokrasia, Kijamhuri, Kidikteta, Kifalme hutunga sheria ambazo ni za kiholela, zinazobadilika kulingana na wakati, ambazo huridhisha wingi wa kura kama malipo ya kuchaguliwa, zinazowatuza washawishi waliofadhili uchaguzi wa madaraka yao, ambayo hushibisha tamaa zao mwenyewe. Zaidi ya hayo, mahakama inayodhaniwa kuwa huru inaweza kutoa uamuzi tofauti kwa dhurufu zile zile kiholela na kwa ubaguzi. Kwa mfano, vifungu ndani ya Katiba ya India Kifungu cha 370 kinachohusiana na haki maalum za Kashmir kilitumiwa na mahakama ili kuunga mkono wakati wa enzi ya chama cha Congress, lakini ikavipiga marufuku wakati wa enzi ya chama cha BJP. Bila kusahau unyanyasaji na ufisadi unaotokana na kutojali kuhesabiwa Siku ya Kiyama na Mwenyezi Mungu (swt), ambapo mtawala wa watu ndiye mwenye hesabu kubwa. Ambapo katika Uislamu Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt) inayotolewa na dalili za kina ndani ya Quran na Sunnah ndio msingi wa sheria, ina kanuni za fiqh za kuvua utekelezaji maalum wa sheria hizo ambao inafaa kwa kila zama na mahali, inayotazamwa kama uaminifu mkubwa juu ya watu na kutahadharishwa kwa kiwango cha juu cha kuhesabiwa Siku ya Kiyama ili kujiepusha na unyanyasaji na ufisadi.

4. Waislamu wanapaswa kutambua kwamba sheria nyingi na maamuzi ya mahakama yanazofanyika sehemu mbalimbali za dunia, kama vile India, Palestina, Tunisia, Jordan, Uingereza, Ufaransa, Marekani (na kwengineko) zinaafikiana na maagizo ya Umoja wa Mataifa ya CEDAW ambayo yanaangalia kwa chuki dhidi ya utekelezaji Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt) kwa ajili ya wanadamu, wakati huo huo inashajiisha sheria zilizokatazwa na Mwenyezi Mungu (swt). Hivyo ndivyo hali ilivyo kuhusiana na mirathi, ndoa, talaka, hijab na mengineyo. Msimamo mbaya unaoonyeshwa na serikali kote duniani ni uwakilishi wa wazi wa utawala wa Kimagharibi (au Urasilimali) wa ulimwengu unaouweka ‘uliberali’ (wa aina zote) juu ya Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt) chini ya pazia la ‘Usekula’. Sio tu kuathiri Uislamu na utendaji wake bali ni tishio kwa dini zote, lenye thamani ya dhati.  

5. Waislamu wanapaswa kutambua kwamba tangu kuvunjwa kwa Khilafah, mnamo tarehe 28 Rajab 1342 H (miaka 101 Hijria iliyopita), ulimwengu ulipoteza utawala (hukm) wa Mwenyezi Mungu (swt) duniani, Umma wa Kiislamu ulipoteza ngao yake. Fauka ya hayo, mfumo wa utawala wa Khilafah unadhamini utekelezaji wa imani za kidini kwa Dhimmi (wasiokuwa Waislamu ndani ya dola ya Khilafah) kama jambo lililowekwa ndani ya Shariah. Na iwapo Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt) itatishiwa na wajinga miongoni mwa wanadamu, Dola ya Khilafah inatarajiwa kutoacha kutumia gharama yoyote, majeshi na silaha ili kuondoa vitisho hivyo.

Hizb ut Tahrir inawausia na kuwatahadharisha watawala wa India na ulimwengu. Kuweni na busara katika vitendo vyenu kuhusiana na mambo ya Waislamu. Kuregea kwa mfumo wa utawala wa Khilafah kumekaribia kama ilivyothibitishwa na hadith ya Mtume (saw). Tunathibitisha kujitolea kwetu kuhesabu kila ukiukaji wa Shariah ya Mwenyezi Mungu (swt). Ama kuhusu kuhesabuwa na Mwenyezi Mungu (swt) Siku ya Kiyama, ni jambo la yakini madhubuti lililo dhahiri mithili ya mwangaza wa mchana.

 (وَسَيَعْلَمُ الَّذِينَ ظَلَمُوا أَيَّ مُنْقَلَبٍ يَنْقَلِبُونَ)

“Na wanao dhulumu watakuja jua mgeuko gani watakao geuka.” [Al-Shu'araa: 226]

Afisi Kuu ya Habari
ya Hizb ut Tahrir

Hizb-ut Tahrir: Afisi ya Habari
Afisi Kuu ya Habari
Address & Website
Al-Mazraa P.O. Box. 14-5010 Beirut- Lebanon
Tel: 00961 1 30 75 94 Mobile: 00961 71 72 40 43
www.hizb-ut-tahrir.info
Fax: Telefax
E-Mail: media (at) hizb-ut-tahrir.info

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.