Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

Kwa: Waziri wa Usalama wa Ndani na Ushirikiano wa Serikali ya Kitaifa

Kwa: Waziri wa Afya

Kwa: Maimamu wote, Wadau wote wa Kiislamu na Jamii ya Kiislamu

KUH: OMBI LA KUTAKA MISIKITI IFUNGULIWE

Huku janga jipya la virusi vya Korona likiendelea kutikisa nchi na ulimwengu kwa ujumla, serikali ilitoa amri ya kuifunga misikiti yote humu nchini, hatua iliopelekea kusitishwa ndani yake kwa swala za Jamaa na ile ya Ijumaa kwa kipindi cha takriban miezi miwili sasa. Marufuku hii iliyotolewa mwezi March,2020, ambapo kisa cha kwanza cha Covid-19 kiliripotiwa nchini hadi sasa inaendelea kutekelezwa sawia ni ile ilani ya kutotoka nje kuanzia saa moja jioni hadi saa kumi na moja alfajiri ambayo sasa imeongezewa muda wake hadi tarehe 6 Juni,2020.

Tunapokiri vyema athari ya janga jipya la maambukizi ya virusi vya Korona humu nchini na ulimwengu kwa ujumla, tunakariri haja ya kuzingatia hatua zote za kuzuia maambukizi ya maradhi haya hatari kwani hii ni sehemu ya mafunzo ya Uislamu kama alivyo teremshiwa na kutekelezwa na Mtume wetu mtukufu (saw) kwa zaidi ya karne 14 zilizopita.

Sisi pia tuna yakini kwamba janga hili la maambukizi ni changamoto kali na mtihani utokao kwa Muumba Mtukufu ili kuwatahini waja wake, hivyo tunapaswa kumgeukia Yeye kwa ikhlasi kwa kutubia na kutii Ufunuo Wake. Kwa muktadha huu, kufungwa misikiti ni jambo linalochukiwa sana katika Dini ya Mwenyezi Mungu na waja wake ambao bila shaka nyoyo zao ni zenye kuungulika kwa maumivu yaliyokuwa makubwa zaidi ndani ya Mwezi mtukufu wa Ramadhan. Kwa masikitiko makubwa, hata kabla ya hatua ya serikali baadhi ya viongozi wa Kiislamu waliamua kuifunga misikiti badili ya kuchukua hatua za tahadhari za kuwafanya wawe salama huku wakiendelea kuswali swala ya jamaa! Cha kuumiza wakaenda mbali zaidi katika kupindisha dalili za Kiislamu zioane na hatua yao hii ya kihatari!

Tungependa kupaza sauti yetu kuhusu kufungwa kwa Misikiti kwa kusema yafuatayo:

Kwanza: Usitishwaji wa Swala za Ijumaa pamoja na swala za Jamaa ni hatua inayogongana waziwazi na mafundisho matukufu ya Dini yetu. Katika kipindi cha kuenea kwa mkurupuko wa maradhi, sheria tukufu ya Kiislamu imetufundisha kwamba kinacho hitajika sio kusitisha swala za jamaa kwa jumla bali ni kuwatenga walio ambukizwa na kuwazuia kuingia misikitini. Hatua kama vile udumishwaji wa usafi, kuvaa barakoa, upimaji wa watu wengi na kuosha mikono pia zanapaswa kuchukuliwa ili kuzuia maambukizi na kusambaa kwa maradhi. Dalili ya haya ni hadith iliyo simuliwa katika Al Mustadarak kutoka kwa Tariq bin Shihab kutoka kwa Abi Musa kutoka kwa Mtume (saw) aliye sema:

«الْجُمُعَةُ حَقٌّ وَاجِبٌ عَلَى كُلِّ مُسْلِمٍ فِي جَمَاعَةٍ إِلَّا أَرْبَعَةٌ: عَبْدٌ مَمْلُوكٌ، أَوِ امْرَأَةٌ، أَوْ صَبِيٌّ، أَوْ مَرِيضٌ»

"Swala ya Ijumaa ni haki ya uwajibu kwa kila Muislamu katika jamaa isipokuwa kwa watu wanne: Mtumwa anaye milikiwa, au Mwanamke, au mtoto au mgonjwa."

Ama kuhusiana na swala za jamaa, Sheria imeeleza bayana kwamba swala hiyo ni faradhi ya kutoshelezana (Fardh ul-Kifayah) ambayo inamaanisha ni lazima itekeleze kwa njia ya kuendelea na angaa baadhi ya watu ili kuepuka madhambi kuiangukia jamii nzima. Abu Dawud amesimulia kutoka kwa Abu Darda (radhi za Mwenyezi Mungu zimshukie) aliye simulia kutoka kwa Mtume (saw) aliye sema:

«مَا مِنْ ثَلَاثَةٍ فِي قَرْيَةٍ وَلَا بَدْوٍ لَا تُقَامُ فِيهِمْ الصَّلَاةُ إِلَّا قَدْ اسْتَحْوَذَ عَلَيْهِمْ الشَّيْطَانُ، عَلَيْكَ بِالْجَمَاعَةِ فَإِنَّمَا يَأْخُذُ الذِّئْبُ مِنَ الْغَنَمِ الْقَاصِيَةَ»

"Hawawi watu watatu katika mji wala mashamba ndani yao ikawa haisimamishwi Swala isipokuwa Shetani huwa amewatawala juu yao, jilazimishe na (swala za) jamaa kwani mbwa mwitu hula mbuzi aliye kuwa peke yake."

Kwa mtazamo huu, tunakariri kwamba amri ya kufungwa Misikiti haikuwa hatua mwafaka kwani imeitumbukiza jamii yote ya Kiislamu katika hatari ya dhambi kubwa kwa kufeli kudumu kuswali swala za jamaa za kila siku na swala za Ijumaa za kila wiki. Hivyo basi, tunaisihi serikali ifungue misikiti haraka iwezekanavyo. Kwa hakika ni jambo lenye kubughudhi kwa Waislamu wenye ikhlasi kuona kwamba serikali hivi karibuni imeruhusu mikahawa kuendesha shughuli zake kwa hoja ya kuchukua hatua ili kuregelea maisha ya kiuchumi huku wakati huo huo ikiendelea kufunga nyumba za ibada ambamo jina la Muumba Mtukufu hutukuzwa.

Pili: Serikali inapaswa kuweka hatua kama vile udumishwaji usafi, kuvaa barakoa, na upimaji wa watu wengi na kuosha mikono ili kuzuia maambukizi ya maradhi haya kwa Waumini. Na endapo yoyote miongoni mwa waumini atagundulika kuwa na ishara za Covid-19, basi azuiliwe kuingia msikitini huku wengine waendelee na swala zao. Ni jukumu la kimsingi kwa serikali kusaidia katika kutoa huduma kama hizi kwa raia wake wanapo kuwa wenyewe hawana uwezo wa kuzipata hasa ikizingatiwa mtiririko wa ruzuku nyingi, fedha na usaidizi kutoka humu nchini na nje ya nchi uliyo pokewa na serikali unao julikana na kila mtu. Lakini tuna imani kwamba misikiti inaweza kwani kuna waumini wenye ikhlasi wanaotamani kurudi misikitini na wako tayari kusaidia utoaji huduma zinazo hitajika.

Tatu: Huku mwezi mtukufu wa Ramadhai ukikaribia kukamilika itakuwa ni janga kubwa vilevile endapo jamii ya Waislamu hawatoweza kuswali swala yoyote ya jamaa ndani ya mwezi huu mzima, bila ya kutaja swala ya Idd ul-Fitr inayoswalia baada ya kumalizika Ramadhan ambayo tuna hamu ya kuiswali kwa jamaa kama inavyo faradhishwa na Uislamu. Hivyo basi, tunasihi kuwa jambo hili lipewe umakinifu na mazingatio ya haraka. Kwa hakika jamii ya Waislamu wamekuwa na subra ya hali ya juu na sasa ni wakati wa kurudi Misikitini pamoja na kuchukua tahadhari zinazostahiki.

Nne: Tunawakumbusha Maimamu, Viongozi wa Kiislamu na Waislamu wote kwa ujumla kwamba ni jukumu lao kupigia debe na kutoa wito wa kufunguliwa Misikiti. Tungependa kuwanasihi kuwa kunyamazia kwao hali hii ya sasa inayo umiza ni matusi kwa Dini na watu wake na ni chuki dhidi yao na watahesabiwa siku ya Kiyama.  Tafadhali simameni na mzungumze ukweli ili  munyanyue hadhi yenu mbele ya Mwenyezi Mungu Mtukufu anaye amrisha kusema ukweli bila ya uoga wala mapendeleo na mutafute daraja za maswahaba watukufu (radhi za Mwenyezi Mungu ziwe juu yao) walio zungumza haki katika dhurufu ngumu zaidi na kunali daraja za juu zaidi baada ya Manabii na Mitume waliotumilizwa kwa wanadamu.

Ewe Mwenyezi Mungu, shuhudia kwamba tumefikisha ujumbe Wako!

#Covid19   #Korona   كورونا#

H. 24 Ramadan 1441
M. : Jumapili, 17 Mei 2020

Hizb-ut-Tahrir
Kenya

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.