Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Jibu la Swali

Ni Nini Kilicho nyuma ya Saudi Arabia Kupunguza Uzalishaji wa Mafuta?

(Imetafsiriwa)

Swali:

Kwa nini Saudi Arabia, ambayo ni kibaraka wa Amerika, ilishirikiana na Urusi katika shirika la OPEC Plus kupunguza uzalishaji wa mafuta kwa kiasi kikubwa, ambayo itasababisha kupanda kwa bei yake, na hii ni kinyume na matamanio ya Amerika? Amerika ilikasirishwa kutokana na uamuzi huu na kutangaza kutathmini upya mahusiano yake na Saudi Arabia: [Biden aliahidi kwamba hii itakuwa na "athari" kwa Saudi Arabia kwa kusimama na Urusi katika kusaidia upunguzaji kupitia kuchukua hatua zinazolenga kutathmini tena uhusiano kati ya Washington na Riyadh. (France 24, iliyochapishwa 10/16/2022)]. Je, hatua hizi zinaweza kuelezewa vipi, ikizingatiwa kwamba Saudi Arabia na mtawala wake halisi, Bin Salman, ni kibaraka wa Amerika? Na matokeo yanayotarajiwa ni yapi?

Jibu:

Kuanza, lazima ikubalike kwamba kile Saudi Arabia na UAE wamefanya ndani ya shirika la OPEC Plus kwa makubaliano na Urusi kupunguza kwa kiasi kikubwa mafuta yanayotolewa sokoni kwa mapipa milioni mbili kwa siku ni uamuzi wa kushangaza kwa Biden na Ulaya, kwani nchi hizi zinafanya juhudi kubwa kusambaza rasilimali za nishati ya Urusi, na kwa hivyo inahitaji haraka kuona rasilimali zaidi za nishati zisizo za Urusi katika soko la kimataifa kama mbadala ili ukosefu wa rasilimali hizo usiakisi bei ambayo imekuwa ghali sana, hasa Ulaya.  Na ili kujua malengo ya Saudi Arabia katika kuchukua hatua hii, ni muhimu kujua uhalisia wa hali ya siasa ya Kimataifa inayozunguka hatua hii:

Kwanza: Mgogoro wa Kawi barani Ulaya

1- [Muungano wa Ulaya umeidhinisha miezi sita iliyopita kifurushi cha sita cha vikwazo dhidi ya Urusi kwa sababu ya vita vyake nchini Ukraine, ambacho kilihusisha marufuku dhidi ya uingizaji wa mafuta kutoka Moscow kuanzia Disemba inayokuja. Hakika, Uingizaji wa Muungano wa Ulaya wa mafuta ya Urusi ulipungua hadi mapipa milioni 1.7 kwa siku Agosti iliyopita, ikilinganishwa na mapipa milioni 2.6 kwa siku mnamo Januari. (The Independent Arabia, 9/12/2022)]. Marufuku hii inahusisha uingizaji wa mafuta ya Urusi yanayopitia kwenye bahari na wala sio yanayopitia kwenye mabomba fulani, na ili kuonyesha kuunga mkono Ulaya, Marekani ililipa nusu ya mafuta ya Urusi ambayo Ulaya ilikuwa imewacha hapo awali (kabla ya kifurushi cha sita cha vikwazo).

2- Kwa upande mwingine, hasa Ulaya, inatatizika kutokana na mgogoro wa kawi unaoongezeka, ambapo gesi na bei za stima zimekuwa maradufu. Hali kama hii imesababishwa na utegemeaji wa juu wa Ulaya, kabla ya vita vya Ukraine, wa rasilimali za kawi za Urusi, na kama siku hizi bei za gesi zinatofautiana mara nne katika Ulaya na Marekani, hii sio hali ya mafuta, kwani bei za mafuta ziko karibu wastani kimataifa, huku bei za gesi zinatofautiana kulingana na uwepo wa mabomba ya kusafirishia au viwanda vya kusindika gesi. Hii inamaanisha kwamba kifurushi cha sita cha vikwazo vya Ulaya dhidi ya Urusi kitapelekea katika upungufu wa ugavi katika Ulaya kwa mapipa milioni 1.4 ya mafuta, na hiki kiwango cha juu kinatarajiwa kupelekea kuongezeka kwa bei za mafuta. Ikiwa tutaongeza kwa haya uamuzi wa OPEC Plus kupunguza viwango vya mafuta kimataifa kwa mapipa milioni 2 kwa siku, bei zitakuwa za juu sana.

Pili: Urusi na athari ya uamuzi huu juu yake

3- Huku nchi za Marekani na Ulaya zikijaribu kunyonga sana uchumi wa Urusi na kuinyima fedha, nchi hizi zingependa kuona mafuta mengi katika masoko ya kimataifa ili kupunguza mapato ya Urusi kutokana nayo, lakini uamuzi wa karibuni wa shirika la OPEC Plus unafanya usambazaji kuwa mdogo, ambao unapelekea katika upungufu wa usambazaji, bei za juu na hayo yananufaisha Urusi kifedha, na hili ndilo ambalo nchi hizi hazitaki. Ni kweli kwamba Marekani ina malengo ya mbali yanayowakilishwa na kufungua mshikamano wa Ulaya na Urusi, yaani, kubadilisha silsila ya usambazaji wa kawi, lakini kusongwa kifedha kwa Moscow pia ni lengo kuu la Marekani, kwa hivyo inastaajabisha kuona Saudia Arabia ikifanya kazi dhidi ya lengo la Marekani.

4- Miongoni mwa malengo hayo ya Marekani na Ulaya, nchi hizi zinajadili kikamilifu kuweka dari juu ya bei ya mafuta ya Urusi, pamoja na gesi. Hii ni kwa sababu nchi hizo zimeona kuwa Urusi, ambayo rasilimali yake ya kawi imepungua kutoka kwa masoko ya Ulaya kutokana na vikwazo, imefanikiwa kufungua masoko mapya ya mafuta yake nchini India, China na nchi nyingine za Asia. Vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Urusi vimeiruhusu Urusi kufidia tofauti hiyo, ikimaanisha kuwa faida ya kifedha ya hazina ya mafuta ya Urusi haijabadilika ikilinganishwa na kipindi cha kabla ya vita dhidi ya Ukraine kutokana na bei ya juu ya mafuta duniani. Ndiyo sababu, wazo la kuweka dari kwa bei ya mafuta ya Urusi ni kuzuia faida kwa Moscow kwa kile kinachobaki. Mafuta yanatosha katika masoko ya kimataifa, kwa hivyo bei inabaki kuwa nzuri kulingana na nchi hizi. Kuweka kikomo cha bei ya mafuta ya Urusi bado kunapangwa, na nchi za Ulaya na Amerika hazijathubutu kuziweka kutokana na athari zake kwa bei ya dunia huku Urusi inajizuia kusambaza mafuta kwa nchi hizo ambazo ziliweka kikomo kwa bei yake ya mafuta.

Tatu: Uchaguzi wa Bunge la Marekani

1- Uchaguzi wa katikati ya muhula wa Bunge la Marekani utafanyika tarehe 8 Novemba 2022. Chama cha Republican, chama cha Rais wa zamani Donald Trump, kinatarajia kushinda chaguzi hizi na kudhibiti mabaraza yote mawili ya Congress; Wawakilishi na Maseneta... na chaguzi hizi ni muhimu kwa sababu matokeo yake ni kielelezo cha uchaguzi wa urais wa 2024 ambapo Chama cha Republican kinapanga kuregea madarakani, na katika mazingira ya mgawanyiko mkubwa ambao Amerika inateseka na kugawanyika kati ya chama cha Democratic na Makampuni ya teknolojia yanayokiunga mkono na kati ya Chama cha Republican na makampuni ya mafuta yanayokiunga mkono, uamuzi wa shirika la OPEC Plus una mwelekeo wa kina kuhusiana na chaguzi hizi, na huu ndio ufunguo wa uamuzi wa Saudi Arabia kuunga mkono kupunguzwa kwa uzalishaji wa shirika.

2- Kuhusu ufunguo huu, ni kwamba Amerika inaishi katika kipindi kigumu sana, yaani mwezi mmoja kabla ya uchaguzi wake: [Mnamo Oktoba 5, muungano wa nchi zinazouza mafuta OPEC + ulitangaza kupunguza uzalishaji wa mafuta kwa mapipa milioni mbili kwa siku, kuanzia Novemba ijayo, huku kulisababisha ongezeko la bei ya mafuta kwa takriban asilimia 10, kabla ya kushuka kidogo wiki hii (Anadolu Agency, 10/12/2022)]. Matokeo haya yasiyoepukika ya uamuzi wa OPEC Plus, yaani, kupanda kwa bei, ndiyo maana ya Saudi Arabia kuunga mkono uamuzi huo, kwa sababu bei ya mafuta nchini Marekani ni nyeti kwa mpiga kura wa Marekani na kwamba kupanda kwake kunabadilisha hali ya mpiga kura huyo na kumuweka mbali na Rais Biden na Chama chake cha Democratic na kumsukuma kuchagua wagombea wa Chama cha Republican. Amerika ilikuwa ikiwasiliana na Saudi Arabia na Mataifa ya Ghuba kuakhirisha uamuzi wa OPEC Plus kwa mwezi mmoja, yaani hadi baada ya uchaguzi wa katikati ya muhula wa Marekani. (Gazeti la Wall Street Journal lilisema kuwa Saudi Arabia ilikataa kujibu maombi ya maafisa wa Marekani ya kuakhirisha uamuzi wa kupunguza uzalishaji wa mafuta ndani ya OPEC Plus.) Gazeti hilo lilisema, likinukuu vyanzo vinavyofahamu mazungumzo hayo, kwamba maafisa wa Marekani, siku chache kabla ya uamuzi huo kuchukuliwa mnamo tarehe 5 Oktoba, iliwaita wenzao katika Ufalme na nchi nyingine za Ghuba zinazozalisha mafuta kutaka uamuzi huo uakhirishwe kwa mwezi mwingine, lakini walikataa. Watu waliohusika na suala hili walisema kuwa maafisa wa Marekani walianzisha kampeni kali ya kuishinikiza Saudi Arabia kuakhirisha mipango yake na maafisa wa Ikulu ya White House wamepiga simu mara kadhaa na Mwanamfalme Mohammed bin Salman, na Waziri wa Fedha wa Marekani Janet Yellen alizungumza na Waziri wa Fedha wa Saudi Arabia, kwa mujibu wa gazeti hilo. (Al Hurra, 11/10/2022). Kwa hivyo, ni dhahiri kwamba uamuzi wa kupunguza uzalishaji wa mafuta ni nyeti sana kwa Chama cha Democratic na kwa utawala wa Biden kabla ya uchaguzi, na kwamba utawala ulijaribu kuakhirisha, lakini haukufaulu!

3- Pamoja na hayo yote kusemwa, ni dhahiri kwamba Saudi Arabia, na uungaji mkono wake madhubuti kwa uamuzi wa OPEC Plus wa kupunguza uzalishaji wa mafuta kwa kiwango kikubwa (mapipa milioni 2 kwa siku), haina mpango wa kuunga mkono hazina ya Urusi, ambayo ni yenye chuki dhidi ya nchi za Magharibi, na haina mpango wa kuzidisha mzozo wa kawi barani Ulaya, kwani haiwezi kusimama dhidi yake isipokuwa mabwana zake huko Washington wataiomba ifanye hivyo, na pia ni wazi kwamba Saudi Arabia inapanga na mabwana zake huko Marekani kuongeza hisa za Chama cha Republican, chama cha Trump; chama kinachofanya kazi kwa ushirikiano na vyama vya nje kugonga maslahi ya chama chengine, hata kama chama hicho chengine kiko madarakani!

4- Utawala wa Biden ulionyesha hasira yake kwa Saudi Arabia na uamuzi wake, [Biden alisema katika mahojiano na CNN, Jumanne jioni, "Kutakuwa na matokeo fulani kwa kile walichofanya (Wasaudi) na Urusi." Aliongeza: "Sitaingia katika kile ningezingatia na kile ninachofikiria. Lakini kutakuwa na - kutakuwa na matokeo." Biden alionyesha kuwa "wakati umefika kwa Washington kufikiria upya uhusiano wake na Ufalme (Saudi Arabia)." (Al-Anadolu, 10/12/2022)]. Pia [katibu wa habari wa Ikulu ya White House Karine Jean-Pierre alisema kuwa Rais Joe Biden amekuwa wazi tangu mwanzo wa utawala wake kuhusu haja ya uhusiano tofauti na Saudi Arabia. Katibu huyo wa habari ameongeza kuwa Washington inakagua uhusiano wake na Saudi Arabia na itafuatilia kile kitakachotokea katika wiki zijazo kwa kushauriana na Congress. Aliongeza uamuzi wa OPEC Plus unaonyesha kuwa Saudi Arabia inashirikiana na Urusi kuhusu sera za kawi (Al-Jazeera Net, 10/12/2022)].

Nne: Ama kile kinachotarajiwa, kinaonekana kama ifuatavyo:

1- Kupunguza kwa OPEC Plus kwa mapipa milioni mbili ya mafuta kwa siku ni uamuzi ambao unaweka shinikizo kubwa kwenye usambazaji wa mafuta. Hata kabla ya uamuzi huu, utawala wa Biden ulikuwa umechukua uamuzi wa kuondoa mapipa milioni moja kutoka kwa hifadhi ya kimikakati ya Marekani kwa muda wa miezi sita, ili kukabiliana na kupanda kwa bei ya mafuta nchini Marekani ili kutodhuru utawala wa Biden katika uchaguzi wa Bunge la Congress na kukabiliana na Urusi, [Rais wa Marekani Joe Biden alitangaza kutolewa kwa mafuta kwa njia isiyokuwa ya kawaida kutoka kwa akiba ya Marekani, na hatua zilizochukuliwa kuadhibu makampuni ya mafuta kwa kutoongeza uzalishaji kutoka kwa kodi zisizotumiwa kwenye ardhi ya shirikisho, kulingana na White House. Ikulu ya White House ilisema: "Baada ya kushauriana na marafiki na washirika, Rais atatangaza kutolewa kwa hifadhi kubwa zaidi ya mafuta katika historia, na kuweka mapipa milioni ya ziada sokoni kwa siku kwa wastani - kila siku - kwa miezi sita ijayo." (CNN Arabia, 3/31/2022)].

2- Pamoja na hayo yote, inadhihirika wazi jinsi Rais wa Marekani anavyojaribu kutuliza soko la mafuta la ndani kabla ya uchaguzi wa Bunge la Congress, wakati Saudi Arabia inakataa ombi la Biden la kuongeza uzalishaji, na hatimaye, mwezi mmoja kabla ya uchaguzi wa Congress, inaunga mkono uamuzi wa OPEC Plus wa kupunguza kwa kiasi kikubwa uzalishaji wa mafuta. Saudi Arabia imefanya zaidi, imeongeza maradufu ya kiasi kilichoagizwa kutoka Urusi, na data ya ufuatiliaji wa Refinitiv Eikon inaonyesha [kwamba Saudi Arabia iliagiza tani 647,000 za mafuta, sawa na mapipa 48,000 kwa siku ya mafuta ya Urusi, ambayo ilipokea kupitia bandari za Urusi na Estonia wakati huo miezi ya Aprili hadi Juni, yaani mara mbili ya kiasi ambacho ilikuwa imeagizwa kutoka kwa mafuta ya Urusi katika kipindi kama hicho cha 2021. (Al Hurra, 7/15/2022)]. Huu ni ushahidi wa njama kubwa iliyofanywa na Saudi Arabia, kwa uratibu wa makampuni ya mafuta ya Marekani na chama cha Republican cha Marekani, kupinga sera ya rais. Ikiwa tutaongeza kwa haya yote mawasiliano yaliyofanywa na wafanyikazi wa zamani wa serikali ya Trump na Saudi Arabia, kama vile Jared Kushner, itabainika kuwa Saudi Arabia inaratibu sera yake ya mafuta na Chama cha Republican cha Amerika, haswa kundi la Rais wa zamani Trump na makampuni ya mafuta ya Marekani yanayotii chama cha Republican, na makampuni haya yana udhibiti wa mafuta ya Saudi.

3- Hakuna shaka kwamba sera hii ya Saudi itaiweka wazi, katika siku zijazo, kwa shinikizo kutoka kwa utawala wa Biden, ambao ulitangaza kuwa uko katika mchakato wa kupitia upya uhusiano wake na Saudi Arabia baada ya uamuzi wa OPEC Plus kupunguza kwa kiasi kikubwa uzalishaji. Hakika, maafisa wa utawala wa Biden wanaunganisha kati ya Saudi Arabia na Urusi: [Rais Biden wa Marekani alisisitiza kwamba "kutakuwa na matokeo" kwa Saudi Arabia kutokana na uamuzi wake ndani ya mfumo wa muungano wa mafuta wa OPEC Plus kupunguza kiasi cha uzalishaji, na akasisitiza kuwa ni wakati wa "kutafakari upya" uhusiano na Saudi Arabia. Huku Msaidizi wa zamani wa Marekani kwa Waziri wa Ulinzi wa Masuala ya Umma, John Kirby, akithibitisha kwamba rais aliamuru "tathmini upya" ya uhusiano kati ya Marekani na Saudi Arabia (Al-Hurra, 10/12/2022)], na pia Seneta mwenye ushawishi mkubwa wa Democrat, Bob Menendez, alimshambulia Mwenyekiti wa Kamati ya Mahusiano ya Kigeni katika Seneti ya Saudia, (ikizingatiwa kwamba Riyadh "inaunga mkono kikamilifu Urusi katika uvamizi wake wa kikatili wa Ukraine." Seneta Richard [Dick] Durbin wa Illinois, Jumanne asubuhi, ilisema Saudi Arabia inataka Urusi ishinde vita vya Ukraine,” alisema kwenye kituo cha televisheni cha CNN, “Hebu tuwe wakweli kuhusu hili.” “Ni Putin na Saudi Arabia dhidi ya Marekani.” akisisitiza kwamba Saudi Arabia haikuwahi kuwa mshirika mwaminifu wa taifa letu...” (Al-Hurra, 10/12/2022) Hapana shaka kwamba Saudi Arabia haichukui hatua hizi kwa maslahi ya Urusi, kwani ilikuwa imeweka uzito mkubwa dhidi ya maslahi ya Urusi mnamo 2020 wakati wa utawala wa Trump ili kuishawishi Urusi na kuilazimisha kupunguza uzalishaji (kama ilivyoonyeshwa katika Jibu la Swali la "Mgogoro wa Mafuta na Athari Zake" linalolingana na Aprili 29, 2020), kwa hivyo ikiwa kuna mtu yeyote anayefikiria kuwa Saudi Arabia inaunga mkono Urusi dhidi ya Amerika, hii ni ndoto ambayo haina nafasi kwa watawala wa Saudi Arabia, vibaraka wa Amerika.

Tano:  Huu ndio ukweli wa sera ya sasa ya mafuta ya Saudi Arabia, ambayo inapingana waziwazi na matakwa ya serikali ya Biden, lakini inalingana na matakwa ya Chama cha Republican cha Amerika na kampuni za mafuta za Amerika zinazoiunga mkono, ambayo kutoka upande mmoja inataka kuipandisha bei kwa sababu wananufaika na hilo, na kutoka upande muhimu zaidi wanataka kuwaangusha wafuasi wa Rais Biden wa Democrats katika uchaguzi ujao wa katikati ya muhula wa Congress kwa matumaini kwamba Chama cha Republican kitadhibiti mabaraza yote mawili ya Congress, ambayo yatarahisisha kuregea kwao kwenye Congress ambayo itarahisisha kurudi katika urais pia 2024.

Iwapo Saudi Arabia, pamoja na mataifa ya Ghuba ya mafuta, yangetaka kudhibiti masoko ya mafuta katika suala la masoko na bei, ingekuwa imefanya hivyo kwa maslahi yake na maslahi ya watu wake. Hata hivyo, watawala hawa vibaraka hawafikirii mawazo kama hayo, kwa kuwa wamejifunza ubaraka na kujisalimisha kwa mgeni na wameingiza uadui wa Uislamu na watu wake. Hawatafanya mafuta ya Kiislamu kuwa silaha mikononi mwao, wala mikononi mwa maadui zao isipokuwa kwa Dola inayokuja ya Khilafah hivi karibuni, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

(وَيَوْمَئِذٍ يَفْرَحُ الْمُؤْمِنُونَ * بِنَصْرِ اللَّهِ يَنْصُرُ مَنْ يَشَاءُ وَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ)

“Katika miaka michache. Amri ni ya Mwenyezi Mungu kabla yake na baada yake. Na siku hiyo Waumini watafurahi.  Kwa nusura ya Mwenyezi Mungu humnusuru amtakaye. Naye ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.” [Ar-Rum: 4-5]

21 Rabii’ al-Awwal 1444 H

17/10/2022 M

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.