Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Pendekezo la Marufuku ya Hijab Shuleni nchini Denmark Laonyesha kwa Mara Nyingine Mstari Wazi Kati ya Usekula na Ufashisti

(Imetafsiriwa)

Habari:

Mnamo tarehe 25 Agosti, Tume iliyoteuliwa na serikali ya Denmark ilipendekeza kupigwa marufuku kwa wasichana kuvaa Hijab katika shule za msingi kote nchini. Marufuku hiyo, ambayo inatokana na dhana ya chuki na isiyo na ushahidi kwamba wasichana wadogo wa Kiislamu wanalazimishwa na familia zao kuvaa Hijab, ingetumika katika shule za msingi za umma, za kibinafsi na za bure. Tume hiyo ilisema kuwa kuvaa Hijab kunaashiria wasichana wa Kiislamu kuwa tofauti na wasichana wengine wa Denmark, ingawa hakuna sera ya sare katika shule za umma nchini Denmark na wanafunzi wanaruhusiwa kuvaa wapendavyo. Tume hiyo pia ilipendekeza udhibiti mkali wa shule huru za Kiislamu na ikasema kwamba makundi katika shule za chekechea yanapaswa "kuakisi idadi ya watu" na kwamba lazima kuwe na kozi kuhusu njia za Kidenmark za kulea watoto kwa wazazi "maalum" wa makabila madogo. Malengo yaliyotangazwa na Tume ni kutoa mapendekezo kuhusu: “jinsi sisi nchini Denmark tunaweza kuhakikisha kwamba wanawake walio katika asili za wachache wanaweza kufurahia haki na uhuru sawa na wanawake wengine wa Denmark,” jambo ambalo linachekesha ikizingatiwa jaribio lake la kuwazuia wanawake wa Kiislamu kulea watoto wao kwa imani zao za kidini.

Maoni:

Pendekezo hili ni nyongeza ya hivi punde zaidi kwa safu ya sera za chuki dhidi ya Uislamu na ubaguzi wa rangi zilizotekelezwa nchini Denmark ambazo zimewalenga moja kwa moja na kuwatenga Waislamu na watu wengine walio wachache. Kwa mfano, "Sheria ya Ghetto" ya nchi hiyo inawatenga wahamiaji kuwa 'wamagharibi' na 'wasio-magharibi' na kupelekea kufukuzwa kwa lazima kwa wahamiaji Waislamu na familia nyingine za walio wachache. Mazungumzo ya chuki dhidi ya Uislamu na matamshi ya chuki dhidi ya Waislamu ya wanasiasa wa Denmark na vyama vya kisiasa yamesawazishwa na kuwa ya kawaida, na hukolezwa wakati wa uchaguzi ili kupata kuungwa mkono na sekta ya umma inayokua ya chuki dhidi ya wageni. Bila shaka, uchaguzi mkuu ujao wa Denmark, na mchujo wa serikali ya Social Democrat ya Denmark na vyama vinavyoiunga mkono katika uchaguzi huo, vina sehemu ya kutekeleza katika pendekezo hili la hivi punde la kupiga marufuku hijab kwa chuki ya Uislamu. Nour Olwan, Afisa Mkuu wa Vyombo vya Habari wa shirika, Euro-Med Human Rights Monitor, alisema: “Tunaona mtindo unaokua na hatari nchini Denmark na kote Ulaya kwamba wakati wowote uchaguzi unapokaribia, Waislamu na makabila madogo wanakuwa gunia la ndondi, mbuzi wa kafara au windo rahisi kwa makundi ya kisiasa kupata uungwaji mkono wa watu wengi.”

Wafungaji mkono wa marufuku ya hijab shuleni, wanadai kwa uwongo kwamba vazi hilo la Kiislamu ni aina ya udhibiti wa kijamii wa wasichana wadogo. Hata hivyo, kwa kweli, ni kuzuiwa kwa wasichana wa Kiislamu kuvaa kulingana na imani zao za kidini ambayo ni dhihirisho la udhibiti wa kiimla wa kijamii, na inachochea tu chuki ya Uislamu na unyanyapaa, kutengwa kijamii, ubaguzi na uadui ambao wanawake wa Kiislamu wanakabiliana nao ndani ya jamii. Kulingana na Tume ya Ulaya, utafiti umegundua kuwa kuvaa Hijab kunaweza kuwa kikwazo cha ajira kwa wanawake nchini Denmark. Na utafiti wa Chuo Kikuu cha Stanford wa 2020 uligundua kuwa marufuku ya Hijab katika shule za umma nchini Ufaransa, ilizuia wasichana wa Kiislamu kumaliza elimu yao ya sekondari na njia yao katika soko la ajira.

Haya yote kwa mara nyingine tena yanasisitiza maumbile yasiyotabirika na hatari ya siasa za kisekula na mfumo wa kisekula kwa jumla, ambapo ubaguzi wa rangi na mashambulizi ya kisiasa dhidi ya walio wachache huchukuliwa kuwa chombo kinachokubalika kushinda uchaguzi, na ambapo haki za jumuiya za kidini zinaweza kutupwa kwa matakwa yaliyojengwa juu ya upendeleo na matarajio ya kisiasa ya wale wanaotawala, kama inavyoonyeshwa na marufuku ya hijab na niqab inayotekelezwa katika mataifa mengine ya Ulaya kama vile Ufaransa, Ubelgiji na Uholanzi. Inaonyesha jinsi kuna mstari wazi kati ya utawala wa kisekula na ufashisti, ambapo wale ambao maadili yao yanatazamwa kama 'ya kigeni' kwa idadi kubwa ya watu wanachukuliwa kama raia wa daraja la pili na watoro wa kijamii, na kulazimishwa kutabanni imani na maisha ya kisekula kupitia mkono wa chuma wa sheria. Inapaswa kuwa ukumbusho kwa Waislamu wanaoishi chini ya mfumo wowote wa kisekula au uliotungwa na mwanadamu, kwamba haki zao na imani zao za Kiislamu kamwe hazitalindwa au kuzipata ndani ya dola kama hiyo.

Ni wazi kuona kwamba mfumo wa kisekula umeshindwa kudumisha maelewano kati ya jamii zote na kuhakikisha wale wa imani zote za kidini wanahisi kuheshimiwa na kulindwa. Mfumo wowote unaong’ang’ana kuhimili hisia kali za kidini za raia wake au kulazimisha mtazamo wake wa kimfumo kwa walio na imani tofauti, au pale ambapo haki za wachache wa kidini zinaweza kutupwa kwa msingi wa yeyote aliye madarakani, hakika sio mfano mzuri au thabiti wa utawala.

Marufuku za Hijab shuleni ni sehemu tu ya safu ya sera zinazotekelezwa na serikali za kisekula katika nchi za Magharibi ili kuwaondoa Uislamu vijana wa Kiislamu. Marufuku kama hizo zinatuma ujumbe kwa wasichana wa Kiislamu kwamba wasiwe na haki ya kujitambulisha na mizizi yao ya Kiislamu shuleni, na kwamba wazazi wa Kiislamu hawapaswi kuwa na haki ya kujenga imani na desturi za Kiislamu kwa watoto wao tangu wakiwa wadogo. Kama Waislamu wanaoishi Magharibi, ni muhimu kwamba tuendelee kutoa upinzani kwa nguvu na kusimama dhidi ya majaribio yoyote ya kufifisha kitambulisho chetu cha Kiislamu au kuwaweka mbali vijana wetu na jamii yetu na imani zetu za Kiislamu. Pia tunatakiwa kuwajengea watoto wetu ufahamu wa kina, kuthamini na kujivunia Dini yao ili washike wajibu wao wa Kiislamu kwa kujiamini na kuwatetea kwa hikma na nguvu ya hoja. Na pia tunahitaji kuuwasilisha Uislamu kwa umma mpana zaidi wa wasiokuwa Waislamu kama mfumo badali ya usekula ambao unaweza kupanga mambo ya wanadamu kwa njia ya uadilifu na yenye ulinganifu. Mfano mmoja ni jinsi mfumo wa utawala wa Kiislamu unavyowahakikishia walio wachache wa kidini haki ya kutekeleza imani zao za kidini chini ya ulinzi kamili wa sheria na hauvumilii kuhujumiwa kwa imani yao au madhara ya haki zao za kidini. Haya ni matokeo ya mfumo aliofafanuliwa na Muumba Mjuzi na Muadilifu, Mwenyezi Mungu (swt) badala ya akili za kigeugeu na upendeleo za wanadamu. Mwenyezi Mungu (swt) asema,

(إِنَّ الَّذِينَ قَالُوا رَبُّنَا اللَّهُ ثُمَّ اسْتَقَامُوا فَلَا خَوْفٌ عَلَيْهِمْ وَلَا هُمْ يَحْزَنُونَ * أُوْلَئِكَ أَصْحَابُ الْجَنَّةِ خَالِدِينَ فِيهَا جَزَاء بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ)

“Hakika walio sema: Mola wetu Mlezi ni Mwenyezi Mungu; kisha wakatengenea, hawatakuwa na khofu, wala hawatahuzunika. Hao ndio watu wa Peponi, watadumu humo, kuwa ni malipo kwa waliyo kuwa wakiyatenda.” [Al-Ahqaf: 13-14].

 

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na
Dkt. Nazreen Nawaz
Mkurugenzi wa Kitengo cha Wanawake katika Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.