Jumanne, 09 Ramadan 1445 | 2024/03/19
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Jibu la Swali

Upeo na Umuhimu wa Muungano wa Kijeshi wa Amerika na Uingereza na Australia

(Imetafsiriwa)

Swali:

Ni upi upeo na umuhimu wa muungano wa kijeshi wa Amerika na Uingereza na Australia? Je! Umeelekezwa dhidi ya China? Au ni kichapo cha Uingereza na Amerika kwa Ufaransa baada ya kuharibu ushawishi wa Uingereza nchini Tunisia, na baada ya wafuasi wake kugeuka dhidi ya mawakala wa Amerika nchini Guinea, na baada ya juhudi za Ufaransa kujenga nguvu ya Ulaya ilio huru na Amerika?

Jibu:

Ili kupata jibu wazi kwa maswali haya, tutapitia mambo yafuatayo:

1- Katika mkutano kupitia video, Rais Biden wa Amerika, Waziri Mkuu wa Uingereza Johnson na Waziri Mkuu wa Australia Morrison walizungumza na kutangaza (pande hizo tatu) ushirikiano wa ulinzi. Kulingana na Sky News Arabia, 16/9/2021, Biden alisema: "Sisi sote tunatambua umuhimu wa kuhakikisha amani na utulivu katika Indo-Pacific kwa muda mrefu," na Morrison alisema, "tutaendelea kutimiza yote katika ahadi zetu za NPT.” Johnson, kwa upande mwengine, alielezea uamuzi huo kama "muhimu" na akasema, "Utakuwa moja ya miradi migumu zaidi ulimwenguni." Nchi hizi zilificha utayarishaji wa muungano wao na kisha kuishangaza China na Ufaransa nayo.

2- Ufaransa ilionyesha hasira kali na kuishutumu Amerika na Australia kwa kusema uwongo, na kuituhumu Uingereza kwa upendeleo wa kudumu, na kusema kwamba muungano huu ni sawa na kudungwa kisu mgongoni mwake kwa sababu Australia ilifuta mpango mkubwa wa nyambizi uliosainiwa na Ufaransa tangu 2016 wenye thamani ya euro bilioni 56 (Dolari za Kimarekani bilioni 66 - BBC, 18/9/2021). China pia ilizungumzia juu ya uzinduzi wa kwanza wa vita baridi katika bara la Asia, na ikataka Amerika na Uingereza kukagua utangamano wa muungano huu na Mkataba wa Kuzuia Kuenea kwa Nyuklia kwa sababu kwamba uhamishaji wa teknolojia ya nyambizi ya nyuklia kwenda Australia kama nchi isiyo ya nyuklia inaweza kuwa ukiukaji wa mkataba huo. Hakuna shaka kuwa China itachukulia muungano huu kuwa hatari kwake, haswa kwa nyambizi za nyuklia za Australia, ambazo zinapinga uchokozi wa Wachina katika bahari za Asia.

3- Na ikiwa Ulaya, mshirika wa jadi wa Amerika, amepona mwishoni mwa enzi ya Trump huko Amerika, na afueni hii imeongezeka kwa tamko la rais wa Amerika: "Amerika imerudi tena" ambayo ilichukuliwa kama kauli mbiu yake tofauti na ile ya mbiu Trump "Amerika kwanza". Hata hivyo, utekelezaji wa utawala wa Biden wa kujitoa kutoka Afghanistan bila kuzingatia maoni na masilahi ya Ulaya umeonyesha utegemezi wa fedheha wa nchi hizi kwa Amerika. Kuondolewa kwa Amerika kutoka Afghanistan ilikuwa hatua kubwa zaidi ya kimataifa iliyofanywa na utawala wa Biden katika kipindi cha miezi tisa baada ya kuingia madarakani, akifuatia mtangulizi wake Trump. Baadaye, kulikuwa na ukosoaji mpana wa Amerika huko Ulaya, maarufu zaidi ilikuwa mwito wa Ufaransa wa kujenga na kuimarisha kikosi cha Ulaya kilicho huru na Amerika. Ndipo muungano huu mpya wa Amerika na Australia na Uingereza (iliyojiondoa katika Jumuiya ya Ulaya) ulifanyika, ambao ulifanya mambo kuwa mabaya zaidi! Hii ndio ilimchochea Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa kusema, "Uamuzi huu wa kikatili, wa upande mmoja na usiotabirika unanikumbusha mengi ambayo Bwana Trump alikuwa akifanya," "kukuchoma kisu  mgongoni" na "kukupa pigo chungu." Ufaransa kisha ikamwondoa balozi wake kutoka Washington kwa mashauriano!

4- Kwa kuchunguza kwa uangalifu upeo wa muungano huu mpya wa kijeshi, tunaona kuwa ni tukio kubwa katika uwanja wa kimataifa na litakuwa na athari kubwa ambazo zinaweza kutazamwa katika mfumo wa mkakati wa Amerika wa kuzuia kuongezeka kwa umaarufu wa China na katika muktadha wa Amerika na Uingereza "kuiadhibu" Ufaransa kwa kukiuka mpango wake wa kimataifa na athari zake kwa nchi zingine za Jumuiya ya Ulaya. Hili linaweza kuelezwa kama ifuatavyo:

** Kwa upande wa Wachina:

Sio siri tena kwa nchi, haswa Uchina, kwamba malengo ya kimkakati ya Amerika leo ni kupambana na kuimarika kwa China na kukabiliana na nguvu za kiuchumi kimataifa na hatari zake za kijeshi kikanda. Kwa hivyo, China ilielewa malengo ya muungano huu wa kijeshi tangu ulipotangazwa, ilitangaza kuukataa na ikazungumza juu ya "mawazo ya Vita Baridi" na "upendeleo wa kimfumo". Na kwamba makubaliano hayo yanakiuka "kutosambaa kwa silaha za nyuklia" (msemaji wa ubalozi wa China jijini Washington Liu Pengyu alisisitiza kuwa nchi hizi hazipaswi kuunda kambi za kutengwa ambazo zinalenga au kudhuru masilahi ya vyama vyengine, na jambo muhimu zaidi wanapaswa kufanya ni kuondoa mawazo ya vita baridi na upendeleo wa kimfumo. Al-Jazeera Net 16/9/2021).

Ama kwa China:

A- Bila shaka, inatambua kwamba hatua hii ni kiini cha muungano mpya dhidi yake, ambao uko chini ya maandalizi, sambamba na safu za NATO ambazo ziliundwa dhidi ya serikali ya Umoja wa Kisovyeti. Al-Jazeera akinukuu Washington Post: ("Mkataba huu utaruhusu Australia kumiliki na kuendesha nyambizi za hali ya juu zinazotumia nguvu za nyuklia kuchukua nafasi ya boti za zamani zinazotumia dizeli, ikiipa Australia uwezo wa kukera, ambao Uchina inahitaji kuupigia hesabu, ikiwa kuna mzozo wowote” (Al Jazeera 17/9/2021), ikimaanisha kwamba makubaliano haya yataongeza uwezo wa jeshi la Australia kama moja ya viungo vya Asia dhidi ya China, kwa kuipatia nyambizi za nyuklia na makombora ya meli ya Amerika ya Tomahawk.

B- China pia inafahamu kuwa mkakati wa Amerika wa kupinga kuimarika kwa China haujabadilika na mabadiliko ya tawala huko Washington: Ni kuimarisha nchi zinazopinga Uchina zinazoizunguka na kuweka mipango hatari zaidi kuizunguka. Chini ya jina la kufungua maeneo ya bahari na uhuru wa kusafiri, Amerika inapigania bahari zinazoizunguka China, iwe kwa kuhamisha sekta za kijeshi za Amerika moja kwa moja, au kwa kutoa msaada wa kijeshi wa moja kwa moja na mkubwa kwa viungo vya Asia-Amerika vya kupambana na China, kama Japan, Korea Kusini, Australia, India na wengine. Wakati Amerika inatambua kuwa sera zake za kuzuia kuimarika kwa China zimecheleweshwa kwa sababu ya vita vyake nchini Iraq na Afghanistan, China pia inaona kuwa kuchelewa kwa Amerika kunasababisha Washington kujaribu kukomesha kuimarika kwa China bila vizuizi, na hii ni hatari sana, kwani utawala wa Trump kwa kuweka mbele wazo la kuipatia Japan na Korea Kusini silaha za nyuklia na ahadi ya utawala wa Biden leo kuipatia Australia nyambizi za nyuklia, sera ya Amerika dhidi ya China ni hatari zaidi na haijafungwa tena na mikataba ya kimataifa.

** Kwa upande wa nchi tatu washirika katika AUKUS, ilikuwa tarehe 16/9/2021, kama ilivyoripotiwa na Al-Jazeera:

A- (Maafisa wakuu wa utawala wa Amerika walisema, "Ushirikiano huu wa ulinzi unakuja kutokana na ushawishi mkubwa wa Wachina katika eneo hilo." Rais wa Amerika Joe Biden alisema kuwa mpango wa ulinzi wa AUKUS na Uingereza na Australia utaziwezesha nchi hizi kupata uwezo wa hivi karibuni kwa mazoezi ya kijeshi na kurudisha vitisho vinavyoibuka haraka ...).

B- Na (Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson alisema kuwa kuzindua ushirikiano wa utatu wa ulinzi na Amerika na Australia unakusudia kufanya kazi pamoja kudumisha usalama na utulivu katika eneo la Indo-Pacific. Aliongeza kuwa jukumu la kwanza la ushirikiano huu litakuwa kuisaidia Australia kupata nyambizi za nyuklia ...).

C- Waziri Mkuu wa Australia Scott Morrison alisema kuwa nchi yake imefuta kandarasi kubwa ambayo ilikuwa imesaini na Ufaransa mnamo 2016, kununua nyambizi za kawaida, kwa sababu inapendelea kuunda nyambizi kwa msaada wa Amerika na Uingereza zenye nguvu ya nyuklia. Morrison ameongeza kuwa nchi yake haitafuti kupata silaha za nyuklia, na itaendeleza ahadi zake za kutoenea kwa silaha za nyuklia ...).

** Kwa upande wa Ufaransa, kulikuwa na hasira na athari za kihemko, kwani walishangazwa na kile kilichotokea:

a- (Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa Jean-Yves Le Drian alielezea kusitishwa kwa makubaliano ya ununuzi wa nyambizi na Australia kutoka katika nchi yake kama kuchomwa kisu mgongoni, na akaongeza katika taarifa kwa redio ya Ufaransa Info kwamba Ufaransa inahisi kusalitiwa, hasira na uchungu kwa sababu ya Australia kufuta mpango huo, na kuanzisha ushirikiano na Amerika na Uingereza, ambapo kulingana nao, itapata nyambizi zenye nguvu za nyuklia, (Al Jazeera 16/9/2021)). Alisema pia katika taarifa: (“kutokana na pendekezo la rais wa taifa, nimeamua kuwaita mara moja mabalozi wetu kutoka Amerika na Australia. Uamuzi huu usiotarajiwa ni wa haki kutokana na uzito wa uamuzi usiotarajiwa ambao Australia na Amerika ziliutangaza mnamo Septemba 15,” (Euro News Arabic, 17/9/2021) Le Drian aliambia redio ya Ufaransa Info: "Nina hasira ... ni jambo ambalo haliwezi kufanywa kati ya washirika ... ni kupigwa kofi usoni" (Deutsche Welle, Germany, 17/9/2021) na kabla ya uamuzi wa kuwaita mabalozi hao wawili, mamlaka ya Ufaransa ilisitisha hafla iliokuwa imepangwa kufanyika, jana Ijumaa, jijini Washington kuadhimisha kumbukumbu ya vita vya mwisho vya majini wakati wa mapinduzi ya Amerika, ambapo Ufaransa ilichukua jukumu kubwa. (Al Jazeera Net, 18/9/2021).

b- Waziri wa Vikosi vya Wanajeshi wa Ufaransa, Florence Parly, alizingatia kuwa ("Australia kusitisha kandarasi kubwa ya kununua nyambizi za kawaida kutoka nchi yake ni hatari na inaweza kuwa habari mbaya sana ..." (Al-Jazeera, 16/9 / 2021).

5- Ama kuhusu ni kwa nini nchi tatu, zilizoongozwa na Amerika, zilichukua hatua hizi kando na Ufaransa, lakini badala yake na kile kinachofanana na adhabu kwa Ufaransa, yafuatayo yanajulikana:

a- Ufaransa ilikuwa ikikosoa waziwazi na kukataa sera za utawala wa Trump, na hii ilidhihirika katika mgogoro wa mashariki mwa Mediterania kati ya Uturuki na Ugiriki, na wakati utawala wa Biden ulipowasili na kujiondoa kutoka Afghanistan kwa njia hiyo ambayo ilifichua kiwango cha utegemezi wa nchi za Ulaya kwa Amerika, nchi hizo zilitaka kuonekana kama washirika na sio wafuasi, Ufaransa imerudi ndani ya Jumuiya ya Ulaya kushinikiza kuundwa kwa jeshi la Ulaya lililojitenga na mwavuli wa Amerika "NATO", ambayo ni kwamba ilirejea kupinga uongozi wa jeshi la Amerika wa nchi za Ulaya, na imeongeza ujasiri wake dhidi ya ushawishi wa Amerika barani Afrika, ambayo baadaye ilionekana katika mapinduzi ya Guinea na kabla yake katika shughuli za jeshi la Ufaransa katika nchi za Sahel za Afrika, na hii yote imeunda chuki ya Amerika dhidi ya Ufaransa.

b- Baada ya mazungumzo ya Uingereza ya Brexit na nchi za Jumuiya ya Ulaya, ilidhihirika kwamba uhusiano wa Uingereza na Ufaransa ulikuwa umedorora sana, na hakuna hata moja ya nchi hizo zilizoonyesha ishara za kwisha, na hii ilionekana katika mkanganyiko wa Ufaransa na Ulaya kwa maneno na makubaliano ya kuondoka kwa Uingereza kutoka Jumuiya ya Ulaya. Labda Ufaransa na nchi za Jumuiya ya Ulaya nazo zinataka kuzuia nchi zingine katika Umoja kufuata mfano wa Uingereza, na kuondoka katika muungano na muungano kuvunjika, lakini hii imeacha kuzorota mno katika uhusiano wa Ufaransa na Uingereza, na sera zao za kimataifa kwa kiasi kikubwa kutengana. Na wakati Ufaransa iliweza kuchukua madaraka nchini Tunisia kupitia hatua za hivi karibuni za Kais Saied, na zaidi ya hayo kutozingatia masilahi yoyote ya Uingereza, ilianza kutafuta msaada wa Amerika dhidi ya Uingereza nchini Tunisia, na hiyo haikuwa kawaida katika ya sera zao.

c- Kabla ya hapo, mwanzoni mwa Mei 2021 kulikuwa na shida ya kisiwa cha Jersey, ambacho ni kisiwa cha ufalme wa Uingereza na kiko karibu kilomita 20 kutoka bara la Ufaransa, ambapo Uingereza ilituma meli za kivita kuzuia wavuvi wa Ufaransa kuingia Sehemu za uvuvi za Uingereza baada ya kujitoa katika muungano, na Ufaransa ilitishia kukata umeme kutoka kisiwa hicho na kutuma polisi na walinzi wa boti kuwalinda wavuvi wa Ufaransa kufuatia hatua za Uingereza, na hii yote ilikuwa dalili ya kuonyesha kuongeza kwa kasi kuzorota kwa uhusiano kati ya nchi hizi mbili, ambao kwa kweli unasukuma Uingereza kuelekeza kichapo kwa Ufaransa na kuchochea Amerika dhidi yake. Lakini kulingana na desturi ya Uingereza na uovu wake, yote haya ni ya siri ... Kulingana na gazeti la Amerika, The New York Times, serikali ya Uingereza ilikuwa (imecheza dori ya mapema katika kuunda ushirika wa pande tatu na Amerika na Australia kupeleka nyambizi zinazotumia nguvu ya nyuklia katika Bahari ya Pacifiki, kwa mujibu wa maafisa wa London na Washington. (Al Arabiya Net, 19/9/2021)).

D- Lakini lilo hatari zaidi kuliko hili na lile, haswa kwa Amerika, ni mtazamo wa Ufaransa wa kupenda vita kwa Uchina, ambayo ni kinyume na msimamo wa Amerika, (Paris ina hofu kubwa kwamba washirika wake wa jadi watachukua mkakati wa kupingana na China ambao bila shaka utahatarisha masilahi ya Ufaransa katika eneo hilo. Kuteleza kokote kwa kijeshi katika mkakati wa Muungano wa Watatu katika Indo-Pacific kunaweza kusababisha tishio kwa usalama wa raia milioni moja wa Ufaransa huko New Caledonia na Polynesia-Ufaransa, wilaya mbili muhimu za Ufaransa katika zile zinazojulikana kama maeneo ya ng'ambo…) na kwa hivyo inatarajiwa kuwa Ufaransa (itaunganisha dira huru ya kimkakati ya Ulaya wakati itakapopokea urais wa Jumuiya ya Ulaya mwanzoni mwa mwaka ujao na kuendelea na juhudi zake za kuiondoa Ulaya kutoka kwa mwamvuli wa ulinzi wa Amerika na kuimarisha mguu wa Umoja wa Ulaya katika uwanja wa kimataifa kuwa nguvu ya ulimwengu ... (Al-Jazeera, 22/9/2021)).

6- Huu ndio upeo na umuhimu wa muungano huu mpya ambao Amerika, pamoja na ushiriki wa Uingereza, ulifanya kazi kujenga na Australia kuwa kiungo katika kuzingirwa kwa China kwa upande mmoja, na kwa upande mwengine kuichapa pigo kali Ufaransa kwa Australia kusitisha mpango wake wa kuundiwa nyambizi na Ufaransa na kutoijumuisha katika muungano huu. Muungano huu unasukuma maswala katika bahari zinazoizunguka China katika vita zaidi na mzozo, na inathibitisha maoni ya hatari kubwa ambayo Washington inashikilia kukomesha kuimarika kwa China. Kwa upande wa Ufaransa, na sera yake ovyo, ni dhaifu sana kuzizuia ngumi za Amerika na Uingereza usoni mwake. Hakika, nchi zote za Jumuiya ya Ulaya zinakabiliwa na udhaifu mkubwa. Nguvu ya Ulaya ambayo Ufaransa ilitaka kuanzisha kama nguvu ya Ulaya iliyojitenga na NATO ilikuwa ndogo sana (wanajeshi elfu tano) kuonyesha uwezo mdogo wa kimataifa wa Ulaya, haswa baada ya Uingereza kujiondoa katika Umoja wa Ulaya.

7- Kwa hivyo ... hakuna maadili ya kudumu kwa nchi hizi zinazoitwa nchi kubwa leo

[بَأْسُهُمْ بَيْنَهُمْ شَدِيدٌ تَحْسَبُهُمْ جَمِيعاً وَقُلُوبُهُمْ شَتَّى ذَلِكَ بِأَنَّهُمْ قَوْمٌ لَا يَعْقِلُونَ]

“Wao kwa wao vita vyao ni vikali. Utawadhania kuwa wako pamoja, kumbe nyoyo zao ni mbali mbali. Hayo ni kwa kuwa wao ni watu wasio na akili." [Al-Hashr: 14]

Ni dola zinazooza ndani kwa ndani na uhusiano kati yao unaharibika, na labda ni dalili njema ya njia ya Mwenyezi Mungu (swt) kuwezesha kudhihiri kwa Dini yake. Hii ndio iliokuwa hali ya Waajemi na Warumi wakati dola ya kwanza ya Kiislamu iliposimamishwa, na hivi ndivyo namna uhusiano kati yao ulivyokuwa, uhusiano wa kimapambano, na uadui dhahiri.

[وَإِذَا أَرَادَ اللَّهُ بِقَوْمٍ سُوءاً فَلَا مَرَدَّ لَهُ وَمَا لَهُمْ مِنْ دُونِهِ مِنْ وَالٍ]

“Na Mwenyezi Mungu anapowatakia watu adhabu, hakuna cha kuzuia wala hawana mlinzi yoyote badala yake.” [Ar-Ra’d: 11]

18 Safar Al-Khair 1443 H

25/9/2021 M

                                                                                                                                                                    

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu