Alhamisi, 18 Ramadan 1445 | 2024/03/28
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Jibu la Swali

Athari za Mkutano wa Amerika na Urusi Jijini Geneva

(Imetafsiriwa)

Swali:

Mnamo siku ya Jumatano tarehe 16/6/2021 mkutano wa kwanza kati ya Rais Biden wa Marekani na Rais Putin wa Urusi ulifanyika jijini Geneva. Je! Umuhimu wa mkutano huu ni nini? Na lengo lake ni nini? Je! Matokeo mazuri yalipatikana kutoka kwa mkutano wa marais hao wawili huko Geneva, ambayo ni kwamba, je! Uhusiano wa Amerika na Urusi unaelekea kuboreshwa baada ya miaka ya kuelezewa kuwa mbaya zaidi katika historia ya nchi hizo mbili?

Jibu:                                   

Athari za mkutano wa Amerika na Urusi zinaweza kueleweka tu kwa kuelewa asili iliyosababisha kuzorota kwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili katika miaka ya hivi karibuni:

1- Vyombo vingi vya habari na wanasiasa wengine wanaelezea nchi hizo mbili, Amerika na Urusi kama "mazimwi mawili," ikiwa ni mwendelezo wa uhalisi ambao umeingizwa akilini; kwamba Amerika na Umoja wa Kisovieti ni nchi mbili zenye nguvu na kubwa zaidi ulimwenguni, kila moja ina kambi. Ukweli ni kwamba, udhaifu mkubwa uliolikumba jimbo la Urusi baada ya kuanguka kwa Umoja wa Kisovieti, umepunguza sana nafasi yake kutoka kiwango cha ushindani wa kimataifa na Amerika. Kwa haya yote, mkutano uliofanyika kati ya wakuu wa nchi hizi mbili hauna umuhimu sana kuliko mkutano wa kilele wa US-Soviet, ambao ulikuwa na athari nyingi, kwani ni nguvu ya jeshi tu, haswa uwezo wa nyuklia na makombora, na uwezo wake wa satalaiti katika anga ulibaki kutoka nguzo za ukuu wa Urusi! Vinginevyo, Urusi haina ukuu.

2- Uhusiano wa Urusi na Amerika ulianza kuzorota kwa kumalizika kwa utawala wa Obama, kwani vikwazo (vilivyowekwa) vilitokana na uvamizi wa Urusi wa Crimea mnamo 2014 na kufukuzwa kwake kutoka Kundi la Nane Kuu (G8), kisha vikwazo kwa sababu ya kuingilia katika uchaguzi wa Amerika mnamo 2016, na utawala wa Obama kufukuza wanadiplomasia 35 wa Urusi na kuweka vikwazo kwa huduma za ujasusi za Urusi mwishoni mwa Disemba 2016, ambayo ni, baada ya Trump kushinda uchaguzi wa Amerika na kabla ya kuchukua majukumu yake (Deutsche Welle , 14/1/2017). Licha ya maneno matamu ambayo Trump alitamka kumwelekea Putin, Amerika iliendelea kuweka vikwazo zaidi kwa Urusi, na kushinikiza mvutano katika uhusiano wao na balozi za Urusi kufungwa katika miji mingi ya Amerika, na kulazimishwa vizuizi kwenye vituo vya habari vya Urusi nchini Amerika, na Amerika kuweka vikwazo visivyo muda dhidi ya Urusi na si kwa sababu nzuri, hivyo viliwekwa kwa kukamatwa kwa kiongozi wa upinzani wa Urusi Navalny, mashtaka yaliwekwa kwa kumpa sumu mpinzani wa Urusi Skripal nchini Uingereza mnamo 2018, na kushtakiwa kwa kampuni za kiteknolojia za Urusi kwa mashtaka ya shambulizi la mtandao, kufikia mwisho wa utawala wa Trump. Na wakati utawala wa Biden ulipokuja, ulizidisha zaidi mvutano. Rais wa Amerika Biden alimtaja Rais wa Urusi Putin kama "muuaji" na kwamba atalipa gharama kwa kuingilia kwake katika uchaguzi wa Amerika (Sky News Arabic 17/3/2021). Balozi wa Urusi aliondoka Washington kutokana na hayo Machi 2021, kisha balozi wa Amerika akaondoka Moscow mwezi uliofuata ... Amerika ilitishia kuifukuza Urusi kutoka kwa mfumo wa fedha wa kimataifa.

3- Utawala wa Kidemokrasia wa Biden unachukia zaidi Urusi na Rais wake Putin na unamtuhumu kuwa sababu ya Hillary Clinton kushindwa uchaguzi wa urais wa 2016. Wanademokrasia katika upinzani walikuwa wakimtaka Rais wa zamani Trump aiadhibu Urusi wakimtuhumu kuwa mpole nayo, na walikuwa wakimuaibisha kwa hilo na waliitishia Urusi (kwa yatakayowapata) ikiwa watashinda uchaguzi mnamo 2020. Wakati rais wa Democrat Biden aliposhinda katika uchaguzi huo ilisadifiana na shambulizi kali la kimtandao dhidi ya mifumo ya kampuni ya SolarWinds ambayo hutumiwa na mashirika nyeti ya serikali ya Amerika. Ujasusi wa Amerika ulishutumu Urusi kwa mashambulizi haya ya kimtandao ... na Amerika ilianza kuitaja Urusi kama "adui" ... na hata siku mbili kabla ya mkutano huo, Biden alitishia kujiunga na Ukraine katika NATO! Kwa hivyo, mkutano huu haukuendana na mvutano kati ya nchi hizo mbili, lakini ulikuwa na sura nyingine. Kwa kuchunguza asili yake na mwendo wake, inadhihirika kuwa:

a- Mkutano kati ya marais hao wawili ulimalizika kwa saa mbili na nusu licha ya kupangiwa masaa manne, na mkutano wa pamoja na waandishi wa habari wa marais hao wawili haukufanyika, kila mmoja wao alifanya mkutano wake na waandishi wa habari kando, mikutano yote miwili ilipeperushwa na Kituo cha Al-Jazeera mnamo tarehe 16/6/2021 na vyombo vingine vya habari, moja kwa moja, na taarifa hiyo ya pamoja ilipunguzwa kwa makubaliano ya pande hizo mbili kwamba hakuna mshindi katika vita vya nyuklia ingawa haionekani katika upeo kati yao, na Rais wa Amerika Biden aliahidi kuendelea kujitolea kwa Washington kwa Mkataba wa START III kupunguza silaha za kimkakati baada ya kamati ambazo zilikubaliwa kuundwa kukamilisha mahitaji ya kwanza katika suala hili. Maswala mengi ya ugomvi kati ya nchi hizi mbili yalizungumziwa, na Rais wa Urusi alimuuliza mwenzake wa Amerika juu ya kumtaja kama "muuaji." Biden alizungumza katika mkutano wake na waandishi wa habari juu ya athari mbaya za kifo cha kiongozi wa upinzani wa Urusi Navalny gerezani, lakini aliusifu mkutano huo kuwa wenye matunda na mzuri na alikiri kisiri kwamba mkutano huo ulijumuisha tishio kwa Urusi ikiwa itaingilia uchaguzi wa Amerika tena au kufanya mashambulizi ya kimtandao tena. Rais wa Urusi alisema katika mkutano wake na waandishi wa habari kuwa ni vigumu kusema kuwa uhusiano kati ya nchi hizi mbili unaboreka, lakini alizungumzia mwangaza wa matumaini kwa hilo, na aliishambulia Amerika katika suala la Haki za Binadamu akikumbuka magereza ya Ujasusi ya Amerika huko Guantanamo na nchi zingine na tabia mbaya za Amerika dhidi ya watu weusi na mataifa mengine; hii ni kutokana na ukosoaji mkali wa Amerika juu ya haki za binadamu nchini Urusi. Biden alizungumzia umuhimu wa kufanya mkutano wa moja kwa moja kati yake na Putin ili kuepusha sintofahamu yoyote katika uhusiano kati yao, na kuelezea kwamba mustakabali wa uhusiano unategemea hatua za Urusi.

b- Baada ya kutathmini, tunaona kwamba Amerika ndiy aliyochukua hatua ya kuishinikiza Urusi, na Amerika ndiyo iliyoongeza mvutano kati yao kwa kiwango ambacho Rais Putin wa Urusi aliwataja hapo awali kuwa "mabaya kwa Urusi", Amerika ndiyo aliyoanzisha mkutano wa kilele kati ya viongozi hao wawili bila kuwa na makubaliano juu ya hoja za ugomvi kati yao, na Urusi ilifurahi kwamba Biden ndiye rais wa kwanza wa Amerika kuamua kukutana na rais wake katika ziara yake ya kwanza ya kigeni, kama ushahidi kwa Urusi jinsi Washington inavyoishikilia kwa umuhimu Moscow. Rais Biden wa Amerika aliijibu kwa kutembelea Uingereza na kukutana na Waziri Mkuu wake Johnson, na kufanya Mkutano wa G7 huko Uingereza moja kwa moja, baada ya kutarajiwa kuwa mtandaoni. Biden aliongezea kuhudhuria mkutano wa NATO jijini Brussels, ambapo alifanya mikutano kadhaa, pamoja na Rais Erdogan wa Uturuki, na huko Brussels, Biden pia alifanya mkutano nadra wa aina yake na wakuu wa Baraza la Ulaya, Charles Michel na Tume ya Ulaya Ursula von der Leyen. Kwa hivyo, mkutano wa Biden-Putin ukawa moja ya mikutano mingi ambayo rais wa Amerika alifanya kibinafsi katika ziara yake ya Uropa, ikipunguza matumaini ya Urusi ya kuwa na mkutano maalum kwa ajili yake!

c- Kwa haya yote, inaweza kusemwa kuwa matokeo mazuri ya mkutano wa kilele kati ya viongozi hao wawili yalikuwa sahili sana na yalifungamana na kurudisha mabalozi wa nchi hizo mbili kwa mji mkuu wa kila mmoja, na ahadi juu ya START III (Mkataba wa kimkakati wa Kupunguza Silaha), na kwamba uboreshaji wa uhusiano kati yao unategemea hatua zifuatazo za Urusi, yaani, maridhiano na makosa, kama zile zilizokuwa katika dosari la kimkakati la Urusi kuisaidia Amerika nchini Syria. Pamoja na tangazo la Rais Putin la uingiliaji wake wa kijeshi huko Syria baada ya mkutano wake na Rais wa Amerika Obama jijini New York mnamo 28/9/2015, Urusi ilikuwa imetoa huduma zake za kijeshi kwa niaba ya Amerika, na labda Urusi ilichochewa na chuki yake dhidi ya Uislamu na Waislamu kupigana nchini Syria, na labda pia ilikimbilia kukomesha kutengwa kwake kimataifa baada ya kuikamata Crimea mnamo 2014 na vikwazo vya Magharibi, lakini muhimu zaidi ni kwamba Amerika imeonja huduma za jeshi la Urusi na kuona umuhimu wao katika kutumikia ushawishi wake nchini Syria, na kwamba imekuwa ikitamani sana kuhamisha misheni hii karibu na China. Uingiliaji wa Urusi nchini Syria, wakati ilikuwa ikifahamu juu ya utegemezi wa Bashar kwa Amerika, lilikuwa kosa kubwa la kimkakati ambalo hakuna uongozi wa busara wa nchi yoyote huru unaweza kutekeleza.

d- Ama malengo fiche ya Amerika kwa shinikizo lake kwa Urusi, ni kuifanya Urusi kuwa ngazi ya kimataifa katika mkakati wa Amerika dhidi ya China, na ikiwa Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje wa Amerika Henry Kissinger ndiye mwasisi wa ushiriki wa Urusi katika kuweka shinikizo kwa China na kuilazimisha ikae kwa amani na Amerika wakati wa Vita vya Vietnam katikati ya miaka ya sitini, katika karne iliyopita, Mmarekani huyu mwandamizi ametazamwa na duru za kisiasa za Amerika kama mtaalamu wa kisiasa aliye na ufahamu juu ya siasa za kimataifa. Kwa hivyo, mnamo 2016, duru hizi zilimpangia mikutano miwili muhimu na tofauti wakati alikuwa katika miaka ya tisiini na wagombea urais wa Amerika Hillary Clinton na Donald Trump, na mapendekezo yake yalikuwa kwao umuhimu wa kuishirikisha Urusi pamoja na Amerika na kuitumia dhidi ya China.

e- Licha ya ukweli kwamba malengo haya ya Amerika hayajatangazwa, Amerika huwafikishia Urusi kwa njia moja au nyingine na Urusi inaelewa vizuri. Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi Lavrov alisisitiza (kwamba Amerika haitaweza kuigeuza Urusi kuwa chombo cha kutimiza maslahi yake, na kukabiliana na China ... wanajadili sasa, kwa umakini, jinsi ya kuitumia Urusi dhidi ya China kwa faida yao ... kwa hamu ya kutufanya chombo cha kutumikia maslahi ya Amerika." Aliongeza,"Lakini kwa kweli hili halitawezekana kwetu.") [RT 24/12/2018]

f- Na, hili ndilo hasa Amerika inalolitaka kutoka kwa Urusi, kwa hivyo inaishinikiza na hali ni tete mno, katika kutekeleza nadharia ya Henry Kissinger ya kuidhibiti China kwa kuhusisha Urusi. Vinginevyo, Urusi haishindani na Amerika, si katika uchumi wala katika siasa za kimataifa, na hakuna chochote ndani yake cha dola kuu isipokuwa nguvu za kijeshi. Mikataba ya Amerika na Soviet na kisha mikataba ya Urusi iliweka nguvu ya jeshi la Urusi katika mfumo wa nidhamu mbali na tishio kwa Amerika. Kwa kweli, Amerika ilikataa mikataba mingi kama Mkataba wa Anti-Ballistic tangu 1972 na ikaunda ngao yake ya makombora, Urusi haina uchumi wenye nguvu ambao unastahiki kukuza zaidi uwezo wake wa kijeshi sawa na uwezo ambao Amerika inao ... Uwezo wa nyuklia na mikakati ya Urusi haikuwa sababu na kichocheo cha mvutano wa Amerika katika uhusiano nayo. Badala yake, mvutano huu katika uhusiano na Urusi ulikusudiwa kuishinikiza kuondoka kutoka China, ambayo imekuwa kitovu cha tahadhari kubwa kwa Amerika, kwa hivyo Waziri wa Ulinzi Former Patrick Shanahan, alitoa wito kwa makamanda wa jeshi lake kuiangazia China, akisema "China, China, China" (Al-Jazeera Net, 3/1/2019)

g- Hata hivyo, Amerika, kwa kuhujumu uhusiano na Urusi, hadi sasa imeshindwa kuisukuma Urusi dhidi ya China, hasa kwani shinikizo la Amerika kwa Urusi lilifanana na shinikizo lake kwa China katika vita vya biashara, na hii imeunda uhusiano wa Urusi na China .. ikimaanisha kwamba shinikizo la Amerika kwa Urusi kuilazimisha iende nayo dhidi ya China ina matokeo kinyume na kile Amerika inataka, na bila shaka inajua hatari ya njia ya Urusi ya kuungana tena na China ... Kwa hivyo, utawala wa Biden uliamua kuweka kando njia ya "shinikizo" kwa Urusi, na kuibadilisha na njia ya kuipatia "mwanga wa matumaini" kupitia mkutano wa kilele, na kisha kuondoa mapatano kati ya Urusi na China kadiri iwezekanavyo ... na kufungua mazungumzo makubwa nayo kupitia kamati ambazo ziliundwa katika mkutano wa viongozi hao wawili.

4- Kwa hivyo, mkutano wa Biden na Putin ni kufanikisha lengo hili, ambalo ni kumpa mwanga wa matumaini Putin kwa suala la kuondoa mivutano ya Amerika na mashinikizo dhidi ya Urusi kama njia ya kuunga mkono Amerika katika msimamo wake kuhusu China au angalau kuzuia uhusiano wa Urusi na China. Kwa habari ya mivutano mingine kati ya nchi hizi mbili, haistahili umuhimu huo wote, kwa mfano, majadiliano kati yao kuhusu Syria na kwamba Amerika inataka kutatua mzozo wa Syria kama inavyotaka, hii haipingwi na Urusi kwani maadamu inaokoa uso wake, na vile vile nchini Afghanistan, Urusi haiwezi kuifanyia kazi Amerika nchni Afghanistan, kama ilivyoitumia wakati wa miaka ya themanini. Halafu, ikiwa Urusi iliingilia uchaguzi wa Amerika, hii ni kwa sababu ya uwazi wa mtandao kama njia mpya ya ushawishi. Labda Urusi ilidharau nguvu ya athari ya Amerika, vinginevyo ingekuwa imehama kutoka kwa uingiliaji huo. Kwa shambulizi la kimtandao ambalo Amerika inaishtumu Urusi kulitekeleza, halina athari muhimu ambayo ni vigumu kusuluhisha; Biden aliwajibu baada ya mkutano wake na Putin kwamba Amerika ina uwezo mkubwa sana wa kupenya Urusi na kusababisha hujuma za kielektroniki / kidijitali ndani yake ikiwa Urusi itarudi kupenya tena, na akatolea mfano wa uwezo wake wa kuhujumu mabomba ya mafuta ya Urusi…

5- Rais wa Urusi aliondoka Geneva akijua kabisa kuwa Amerika inasubiri hatua zifuatazo za Urusi katika miezi ijayo na kwamba iko katika mchakato wa kuchunguza na kusimamia hatua hizo kupitia kamati za pamoja ambazo uundaji wake umeidhinishwa. Rais wa Urusi anajua vizuri kuwa uwezo wa Amerika kuishinikiza Urusi ni mkubwa na alipata uzoefu wao. Anajua pia kuwa China inaweza kumwacha na kuelekea Magharibi kwa sababu maslahi yake ya kibiashara huko Magharibi ni makubwa zaidi kuliko maslahi yake ya kibiashara na Urusi. Kwa haya yote, miezi ijayo kuna uwezekano mkubwa wa kushuhudia mafanikio katika uhusiano wa Amerika na Urusi, na kurudi kwa mabalozi katika hatua za mwanzo, na kuna uwezekano zaidi kwamba uhusiano wa Urusi na Wachina utachukua njia baridi, kutokana na hali ya joto katika uhusiano wa Urusi na Amerika, hii inaacha ubaridi katika uhusiano wake na China. Ikiwa hili litaafikiwa, basi mpango wa Rais Biden wa Amerika wa kufanya mkutano huo na Rais Putin wa Urusi utakuwa umekomesha uhusiano wa Urusi na China, na Urusi pia imeweka shinikizo kwa China, japo kwa kiwango kidogo kuliko matarajio ya Amerika kulingana na nadharia ya Kissinger. Ikiwa hili halitafanikiwa na uasi ndani ya Urusi ukiongozwa na Putin utaendelea, utawala wa Biden unatarajiwa kuongeza shinikizo lake kwa Urusi maradufu na kuitishia kwa ukanda wa moto kuzunguka Caucasus, ambapo mzozo wa Azerbaijan na Armenia, kisha Ukraine, na msaada wa Magharibi kwake ili kuiunganisha ardhi yake…

Kwa hivyo, nchi hizi dhalimu, zikiongozwa na Amerika, hazifikirii juu ya kile kinachofaa kwa watu, lakini badala yake kile kinachofikia maslahi yao, hata kama ni hatari kwa watu.

 [أُوْلَـئِكَ شَرٌّ مَّكَاناً وَأَضَلُّ عَن سَوَاء السَّبِيلِ]

"Hao ndio wenye mahali pabaya na wamepotea zaidi njia iliyo sawa." [Al-Ma’ida: 60]

9 Dhul Qi'dah 1442 H

20/6/2021 M

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu