Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

Majibu ya Maswali Yaliyo Pokewa kuhusiana na Jibu la Swali: Athari za Virusi vya Korona

(Imetafsiriwa)

Kwa wale walio na maswali kuhusu Jibu la Swali: Athari za Virusi vya Korona. Haya haya ndio majibu ya maswali yenu:

1- Ama kuhusu tofauti kati ya janga hili na tauni, au kati ya virusi vya Korona (COVID-19) na tauni; hakuna tofauti katika upande wa maambukizi. Maradhi ya tauni na virusi vya Korona yanauwezo wa kuambukiza, kama yalivyo umbwa na Mwenyezi Mungu Al-Qawi na Al-Aziz, pasi na kuzingatia ikiwa maradhi haya yanaenezwa kupitia bakteria au virusi. Kwa hivyo katika upande wa uwezekano wa kuambukiza, upo (katika virusi vya Korona), hii ndio sababu hukmu haitofautiani, na hili ndilo lililo angaziwa katika Jibu hilo la Swali. 

2- Ama na swali kuhusu Jibu hilo la Swali kuwa maradhi ya sasa ya virusi vya Korona si ya kutengezwa na wanadamu, hoja kuwa hili lilitegemea ripoti za Kimagharibi, hivyo basi hatupaswi kuzitegemea: jambo hili sio sahihi, kwa sababu upande wa kisayansi unaweza kuchukuliwa kutoka kwa mtu yeyote yule ikiwa kuna ukinaifu wa kutosha kwamba ni sahihi. Na, hivyo basi, hakuna kosa lolote la kutegemea ripoti za Kimagharibi za wanadamu kutoyatengeza maradhi haya ya maambukizi ya virusi vya Korona. Bali, virusi hivi vipo kimaumbile, pasi na kuwa vimetengezwa na wanadamu, kama ilivyo tajwa katika Jibu hilo la Swali. Tunaiona hoja ya kuwepo kwake kimaumbile kuwa yenye nguvu kuliko ile hoja kwamba wanadamu ndio waliovitengeza kwa malengo yao … hususan kwa kuwa maradhi haya yameenea hata katika nchi zinazo tuhumiwa kwa hili, kama China na Amerika … Jibu hilo la swali limetaja yafuatayo:

[Hivyo basi, vita vya maneno vimezuka katika ya Amerika na China kwa sababu ya mkurupuko wa virusi vya Covid-19 (SARS-CoV2), na nchi zote mbili zinatuhumiana kuwa mhusika wa moja kwa moja katika kueneza maradhi haya, na ingawa nidhamu zote mbili zinazo tabikishwa nchini China na Amerika haziwezi kuepushwa kutokana na uwezekano wa kuwa nyuma ya kuenea kwa virusi hivi, lakini, baada ya utafiti kuna uwezekano kuwa hakuna ushahidi wa nguvu kuwa Amerika wala China ndizo zilizo enea maambukizi au kuunda virusi hivi na kisha kuvieneza katika nchi nyenginezo kwa moja ya sababu mbili dhahiri:

Hili limefafanuliwa kwa kina katika Jibu hilo la Swali, ambalo limechapishwa katika ukurasa wa tovuti na laweza kuangaliwa.

3- Swala za Ijumaa ni lazima ziswaliwe ndani ya msikiti na baadhi wa wanachuoni wa fiqh (Fuqaha) wanajuzisha kuswaliwa uwanjani, yaani uwanjani ambapo wanao swali hawatazuiwa kuingia humo. Ama sehemu za kibinafsi, (majumba), rai iliyo sahihi zaidi ni kuwa swala ya Ijumaa haziswaliwi humo na haijuzu. Endapo msikiti au uwanja hauwezi kufikiwa basi zitaswalia majumbani kama swala za adhuhuri rakaa nne, na dola itabeba mzigo wa madhambi kwa kuzuia swala ya Ijumaa kuswaliwa misikitini au uwanjani, kwa sababu nususi zimefafanua jambo hili, na hili linafahamika katika maneno ya Mwenyezi Mungu:

[يَا أيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نُودِيَ لِلصَّلَاةِ مِنْ يَوْمِ الْجُمُعَةِ فَاسْعَوْا إِلَى ذِكْرِ اللَّهِ وَذَرُوا الْبَيْعَ ذَلِكُمْ خَيْرٌ لَكُمْ إِنْ كُنْتُمْ تَعْلَمُونَ]

“Enyi mlio amini! Ikiadhiniwa Sala siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu, na wacheni biashara. Hayo ni bora kwenu, lau kama mnajua.” [Al-Jumu’a: 9].

Muislamu anastahiki kuswali bila ya kuzuiwa

[فَاسْعَوْا إِلَى ذِكْرِ اللَّهِ وَذَرُوا الْبَيْعَ]

“nendeni upesi kwenye dhikri ya Mwenyezi Mungu, na wacheni biashara.” [Al-Jumu’a: 9].

Kuiendea swala hii ni wajib kwa sababu imehusishwa na kuacha jambo la mubah… yaani, swala haifanyiki sehemu za kibinafsi, kama vile majumbani, ambako lililo haramishwa limeruhusiwa … Hii ndio sababu imeelezwa katika Jibu hilo la Swali kuwa kufungwa misikiti na watawala na kuzuia swala misikitini ni jambo ambalo haliruhusiwi na linawabebesha dhambi kubwa watawala hawa. Hivyo basi, endapo watawala watakataza kuswaliwa swala za Ijumaa msikitini, na hakupatikani sehemu nyengine yoyote ya kuswaliwa ila majumbani, basi kutaswaliwa majumbani swala ya adhuhuri rakaa nne, na dola inayo funga misikiti itabeba dhambi kubwa kama iliyo elezwa katika Jibu hilo la Swali.

4- Ama swali: (Basi, leo swala za Ijumaa na Jamaa zimesitishwa kutokana na hofu ya watawala madhalimu, kama ninavyo fahamu, na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi Zaidi) … Hili lahitaji ufafanuzi … katika jibu letu limeeleza:

Na sio wajib kwa yule aliye hofu, kutokana na yale yaliyo simuliwa na Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi naye, kwamba Mtume (saw) amesea:

«مَنْ سَمِعَ النِّدَاءَ فَلَمْ يُجِبْهُ فَلَا صَلَاةَ لَهُ إلَّا مِنْ عُذْرٍ، قَالُوا: يَا رَسُولَ اللهِ وَمَا الْعُذْرُ؟ قَالَ: خَوْفٌ أَوْ مَرَضٌ»

 “Yeyote anaye sikia adhana basi na aitikiye kwani hakuna swala isipokuwa kwa mwenye udhuru. Wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu na ni upi udhuru? Akasema: hofu na maradhi.” Imepokewa na Al-Bayhaqi katika Al-Sunan Al-Kubra… Hofu kama inavyo elezwa katika Al Mughni ya Ibn Qudama 1/451: [(881) mlango wa: mtu anayeiwacha kwa ajili ya hofu anapewa udhuru, kutokana na maneno ya Mtume:

«الْعُذْرُ خَوْفٌ أَوْ مَرَضٌ»

“Udhuru ni hofu au maradhi”. Hofu iko aina tatu, ya nafsi, ya mali au familia. Ya kwanza, ni "kuhofia nafsi yake kutokana na mtawala au adui na mithili yake ambavyo vinaweza kudhuru nafsi…" Pia imeelezwa katika Al Muhazab katika Fiqh ya Imam Ash- Shafi'I na Ash-Sherazi: "…ikiwemo kuhofia madhara dhidi ya nafsi yake na mali yake, au maradhi makali yanayomsibu "hivyo hawezi kuhudhuria", na dalili ya hili, ni yale yaliyo simuliwa na Ibn Abbas, Mwenyezi Mungu awe radhi nao, kwamba Mtume (saw) amesema:

«مَنْ سَمِعَ النِّدَاءَ فَلَمْ يُجِبْهُ فَلَا صَلَاةَ لَهُ إلَّا مِنْ عُذْرٍ، قَالُوا: يَا رَسُولَ اللهِ وَمَا الْعُذْرُ؟ قَالَ: خَوْفٌ أَوْ مَرَضٌ»

“Yeyote anaye sikia adhana basi na aitikiye kwani hakuna swala isipokuwa kwa mwenye udhuru. Wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu na ni upi udhuru? Akasema: hofu na maradhi.”

Yaani, Muislamu amepewa udhuru ikiwa yeye binafsi anafuatiliwa kidhulma na utawala. Endapo atakuwa na yakini au ana kiwango cha chini cha shaka kuwa vibaraka wa watawala msikitini wanamsubiri aje ili wamkamate na kumsababishia madhara, basi hapo anapewa udhuru wa kutoswali swala ya Ijumaa katika msikiti huu, na ni lazima atafute njia ya kuswali Ijumaa msikiti mwengine, ikiwa haiwezekani baada ya kufanya juhudi zote, basi anaweza kuswali adhuhuri rakaa nne sehemu ya faragha… Ikiwa muulizaji amefahamu hivi katika jibu letu hilo, basi ni sahihi, na Mwenyezi Mungu (swt) ndiye Mjuzi Zaidi Mwingi wa Hekima.

5- Hadith,  «لَا عَدْوَى...»“Hakuna maambukizi ...” [Bukhari]

“Kuna wale wanaoifafanua kama kupinga maambukizi … lakini zaidi hii ni habari (Khabar) katika maana ya ombi (Talab). Ikiwa mgonjwa Muislamu ana maradhi ya kuambukiza, yaani yanauwezo wa kuambukiza (wengine), kama yalivyo umbwa na Mwenyezi Mungu (swt), katika hali hii ana udhuru wa kutohudhuria swala ya Ijumaa na Jamaa kwa hofu kuwa wengine wanao swali huenda wakaambukizwa maradhi hayo… Pia ni mojawapo ya nyudhuru zilizo elezwa katika hadith tukufu, «الْعُذْرُ خَوْفٌ أَوْ مَرَضٌ» “udhuru ni hofu na maradhi”.

6- Hadith,

«إِذَا مَرِضَ الْعَبْدُ أَوْ سَافَرَ كُتِبَ لَهُ مِثْلُ مَا كَانَ يَعْمَلُ مُقِيماً صَحِيحاً»

“Pindi mja anapo kuwa mgonjwa au anapo safari, huandikiwa (ujira) mithili ya ule aliokuwa akiupata alipo kuwa mkaazi na mwenye afya njema.” [Bukhari]

Hii ni kuhusiana na msafiri au mgonjwa, yaani yule aliye na udhuru wa kutohudhuria swala za Jamaa na Ijumaa, ataswali kwa mujibu wa Shariah inavyo muelekeza, na atalipwa ujira sawa na wa mkaazi au mtu asiye mgonjwa. Na hivyo basi, hapa haitabikiki kwa mtu mwenye afya njema au mkaazi asiye hudhuria swala ya Ijumaa pasi na udhuru wowote.

7- Ama kupinga kauli yetu kwamba idadi ya chini (ya watu) kwa swala ya Ijumaa ni watatu, na kwamba Al-Shafi'I amesema ni arubaini … haya ni mazungumzo mengine, na taweza kuongeza juu yake kuwa wafuasi wa Imam Maalik wanasema kuwa inapaswa kuwa watu kumi na mbili. Hakuna mgongano hapa, bali kadhia hii haihusiani na kufungwa misikiti ambamo Waislamu wanaswali swala ya Ijumaa na Jamaa, kwa idadi ya watu ya kisheria, kwa kujua kwamba kuna rai ya kifiqhi kuwa watu watatu wanaweza kuswali Ijumaa, kama ilivyo tajwa katika Jibu hilo la Swali.

8- Ama kadhia ya kuchukua sababu (al-Asbab), hiyo ni sahihi, lakini pasi na kukiuka Shariah. Kuchukua sababu hapa itakuwa ni mgonjwa asiende katika swala ya Ijumaa na wenye afya waende … Tumeeleza katika Jibu hilo la Swala (maalumati) ya kutosha kuashiria kwamba misikiti kamwe haipaswi kufungwa ili watu walio na afya waweze kuswali na kwamba hatua zinapaswa kuchukuliwa ili kuwazuia wagonjwa walio na maradhi ya kuambukiza kutokana na kuhudhuria swala, ambapo liko wazi. Haiwezi kusemwa kuwa watu walio na afya huenda wakawa na virusi vya Korona, lakini dalili zikawa hazionekani, na hivyo basi watu wote wazuiwe misikitini, yaani, wakaazi wote duniani wazuiwe misikitini! Haya ni maneno ambayo hayastahiki mjadala wala hata kwa kiasi cha chini cha shaka! Bali, mgonjwa ambaye kwa yakini ana ugonjwa wa kuambukiza ndiye anaye zuiwa, na wale ambao kuna shaka kuwa ni wagonjwa pia wanazuiwa, lakini walio bakia nendeni mkaswali.

9- Ama muulizaji aliye sema kuwa virusi vya Korona havina uti wa mgongo, anamaanisha kama mwanadamu, ndio yuko sahihi … lakini inaonekana kana kwamba mapindo ya ncha zinazo jitokeza katika kiumbe hiki yamelifanya chimbuko la lugha ya Kiingereza kukiita "uti wa mgongo" na maana yake ya Kiarabu "uti wa mgongo" imetumiwa kutokana na kufanana katika miungano ya mifupa katika uti wa mgongo wa mwanadamu … Ndio tukaiweka hivi … na hatukudhani ingekuwa ni mada ya maswali!

10- Kuhusu kuosha maiti … hukmu ya Shariah ni kama ifuatavyo:

a. Rai sahihi zaidi (kutokana na uzito wa dalili) ni kuwa ufaradhi wa kuosha maiti Muislamu ni ufaradhi wa kutoshelezana (Fardh Kifayah), na dalili ya hili ni:

Mtume (saw) alisema kuhusu mtu aliye na Ihram, aliye angushwa na ngamia: «اغْسِلُوهُ بِمَاءٍ وَسِدْرٍ وَكَفِّنُوهُ فِي ثَوْبَيْهِ» “Muosheni kwa maji na (majani ya) mkunazi (Sidr) na mumkafini kwa nguo zake (kwa kuwa alikuwa amevaa Ihram).” [Bukhari ameisimulia kutoka kwa Ibn Abbas].

Na Mtume (saw) aliwaambia wale walio muosha binti yake:

«اغْسِلْنَهَا وِتْراً ثَلَاثاً أَوْ خَمْساً»

“Muosheni idadi ya witri, mara tatu au tano” [Imesimuliwa na Muslim kutoka kwa Umm Atiyah].

- Ni wazi kutokana na Hadith hizi mbili kuwa wale walio tekeleza uoshaji walikuwa ni idadi tu ya Waislamu walio tosheleza (Kifayah), na kwamba Mtume (saw) alitosheka na hilo. Mtume (saw) aliendelea na hukmu hii kwa kila maiti Muislamu aliye kufa zama zake isipokuwa kwa mashahidi katika vita ambao hawakuoshwa, kama vile mashahidi wa Badr na Uhud, ikimaanisha kuwa kuosha maiti ni faradhi ya kutoshelezana (Fardh Kifayah).

b. Hili lilifuatwa na wanachuoni wengi wa kifiqhi (Fuqaha):

Katika Al-Mabsoot ya Surkhasai, inaeleza: “Najua kwamba kuosha maiti ni faradhi, ambayo ni haki ya Muislamu juu ya Muislamu mwengine, yeye (saw) amesema:

«لِلْمُسْلِمِ عَلَى الْمُسْلِمِ سِتَّةُ حُقُوقٍ»

“Kwa Muislamu Juu ya Muislamu mwengine ni haki sita” na zinajumuisha: kuoshwa bada ya kufa kwake, lakini baadhi ya Waislamu watakapo tekeleza, haiwi ni jukumu tena kwa wengine walio salia kwa sababu lile lililo kusudiwa limepatikana.”

- Imam Al-Shafi’i amesema katika “Al-Umm”: “Ni jukumu la watu kumuosha maiti, na kumswalia na kumzika. Hili haliwezi kufanywa na watu wote, na endapo baadhi watalitekeleza, wanao tosheleza, basi litakubalika, Mwenyezi Mungu (swt) akipenda.”

Na katika “Al-Sharh Al-Kabeer” ya Ibn Qudamah: [Mlango wa Kuosha Maiti Suala la Kuosha Maiti, kumzika na kumkafini, na kumswalia ni faradhi ya kutoshelezana] kwa sababu Mtume (saw) alisema kuhusu yule mtu aliye angushwa na ngamia wake:

«اغْسِلُوهُ بِمَاءٍ وَسِدْرٍ وَكَفِّنُوهُ فِي ثَوْبَيْهِ»

“Muosheni kwa maji na (majani ya) mkunazi (Sidr) na mumkafini kwa nguo zake (kwa kuwa alikuwa amevaa Ihram).” [Bukhari na Muslim]

c. Ikiwa maiti hawezi kuoshwa kwa sababu fulani, kama ukosefu wa maji au mwili wa maiti umechomeka vibaya na endapo ataoshwa kwa maji, mwili huo utamomonyoka … au ikiwa amekufa kutokana na maradhi ya kuambukiza kama ukoma, tauni, virusi vya Korona, na maradhi mengineyo, na endapo ataoshwa maradhi hayo huenda yakasambaa hadi kwa muoshaji … hatutaki kutabanni katika hilo, Muislamu na afuate rai ya kifiqhi iliyo sahihi zaidi inayomkinaisha, na nitawanukulia baadhi ya rai za Kishariah za wanachuoni wa kifiqhi:  

- Dhehebu la Hanafi linaona kwamba ikiwa haiwezekani kuuosha mwili kwa maji, kutokana na ukosefu wa maji, basi tayammum kwa vumbi inapaswa kufanywa juu ya maiti, kama ilivyo elezwa katika "Al-Inayah" (16/261). Anasema: “Endapo maiti hawezi kuoshwa, kwa sababu ya ukosefu wa cha kuoshewa, basi tayammum hufanywa kwa vumbi.” Ikiwa haiwezekani kuosha mwili kwa sababu hawezi kuguswa, humiminiwa maji juu yake, kama alivyo sema katika “Maraqi Al-Falah” (224): (Na aliye fura ambaye hagusiki, maji humiminwa juu yake).

- Na dhehebu la Malik linaamini kuwa yeyote ambaye hawezi kuoshwa kwa maji kwa sababu ya kukosekana kwake, tayammum inapaswa kufanywa juu yake … ikiwa kushindwa kuoshwa ni kutokana na vidonda mwilini, malengelenge, ukuju, au tetemaji; na endapo ataoshwa kwa maji itapelekea kuharibika na kumomonyoka, basi maji humiminwa juu yake kwa kiasi kinacho uhifadhi mwili kutokana na kumomonyoka na kunyofoka. Ikiwa haiwezekana kumimina maji juu yake, basi tayammum hufanywa … kama ilivyo elezwa katika “Al-Sharh Al-Kabeer” ya Sheikh Ahmed Al-Dardir juu ya “Mukhtasar Khalil”.

Ama dhehebu la Shafi'I, wanaona kuwa ikiwa maiti hawezi kuoshwa kwa sababu yoyote ile, kama vile ukosefu wa maji au kuhofia kumomonyoka kwa mwili ulio ungua, basi maiti huyo hataoshwa, bali tayammum hufanywa juu yake. Bali, wameelekeza kuwa endapo kuna hofu kuwa muoshaji anadhurika na maiti huyo, basi ni wajib kufanya tayammum. Al-Nawawi (Mwenyezi Mungu airehemu roho yake) amesema katika Al-Majmou’: “Ikiwa hamuwezi kumuosha maiti kwa kukosekana maji au ameungua, na endapo ataoshwa mwili wake utamomonyoka, basi haoshwi na tayammum hufanywa juu yake, tayammum hii ni wajib kwa sababu ni utakasaji na sio uondoaji wa najisi. Hivyo katika kutoweza kutumia maji basi tayammu hufanywa kama katika josho (ghusl) la Janaba. Ikiwa ameumwa, na endapo ataoshwa mwili utamomonyoka, au kuna hofu kuwa muoshaji atadhurika, tayamum hufanywa juu ya maiti…”

Ama dhehebu la Hanbali, wana riwaya mbili, ya kwanza: “Pindi ikiwa maiti hawezi kuoshwa kwa kusuguliwa (mwili) kwa sababu yoyote, maji humiminwa juu yake pasi na kusuguliwa, vyenginevyo tayammum hufanywa…”

Katika riwaya nyengine: (Yeyote ambaye hawezi kuoshwa basi tayammum haifanywi juu yake na huswaliwa bila ya kuoshwa au kufanyiwa tayammum, kwa kuwa lengo la kuoshwa ni kusafishwa, na hilo halipatikani kupitia tayammum).

Sheikh Muhammad bin Muhammad Al-Mukhtar Al-Shanqeeti amesema katika “Sharh Umdat Al-Fiqh”: (Yeyote ambaye ana maradhi ya kuambukiza yanayo dhuru, hii ni kuhusiana na madhara kwa maiti na madhara kwa aliye hai anaye osha maiti, kama ikiwa maiti ana maradhi ya kuambukiza, kupitia utaalamu na ushahidi wa wajuzi, kuwa endapo mtu atamuosha atadhurika, hapo basi tayammum hufanywa…)

Kama muonavyo, hizi hapa rai mbili: Ikiwa Maiti hawezi kuoshwa, tayammum itafanywa juu yake na ataswaliwa na kuzikwa… au ikiwa maiti hawezi kuoshwa, basi tayammum haitafanywa juu yake, ataswaliwa na kuzikwa. Kama tulivyo sema mwanzo wa swali hili, Muislamu afuate rai aliyo kinaika na usahihi wake.

11- Kuhusu nukta kuwa hatutabanni katika masuala ya kiimani na vitendo vya ibada: hili ni kweli isipokuwa katika msingi wa itikadi na ibada zinazo husiana na umoja wa Ummah kama saumu na Idd pindi mwezi mwandamo unapo onekana katika nchi yoyote, pamoja na kadhia hii inayo husiana na kufungwa misikiti, jambo wajib ni kuwa ni lazima ibaki wazi katika nyakati zinazo stahiki kama ilivyo ashiriwa katika Jibu hilo la Swali.

18 Sha’ban 1441 H

11/4/2020 M

#Covid19    #Korona            كورونا#

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumanne, 28 Aprili 2020 20:31
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.