Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Jibu la Swali
Kuziendea Mahakama Katika Dar al-Kufr kwa Ajili ya Kuondosha Ukandamizaji

(Imetafsiriwa)

Swali

Assalamu Alaikum kaka yangu mpendwa. Niko na swali muhimu kwako. Katika Surah Nisaa, aya nambari 60, Mwenyezi Mungu anatuharamisha kufuata hukmu ya kitwaghut. Lakini kwa kukosekana Khilafah, biladi zote za Waislamu zinatawaliwa na viongozi Matwaghut? Kwa hivyo, ikiwa tunahitaji kutatua mzozo wowote, twaweza kwenda katika mahakama za viongozi hao Matwaghut? Lau, mmoja katika wanafamilia yangu atabakwa, je, inajuzu kwenda kutafuta hukmu mahakamani ambako hukmu itafanywa kupitia Taghut ya kidemokrasia? Hawahukumu kwa shariah. Na Mwenyezi Mungu anatuharamisha kwenda kwa Taghut anaye tatua mzozo kupitia sheria yake mwenyewe badala ya shariah ya Mwenyezi Mungu.

Mwenyezi Mungu akulipe kheri kaka.

Jibu

Wa Alaikum Assalam wa Rahmatullahi wa Barakatuh,

Nyuma tulitoa jibu la swali mnamo 18/02/2009, linalo someka:

(Inaruhusiwa kwa wale wanaoishi katika Dar al-Kufr ambako hakuna mahakama za shariah, kwenda katika mahakama za Dar al-Kufr kujiondolea ukandamizaji na kuitetea haki yake, lakini kwa sharti pekee kuwa haki hiyo iwe ni ile aliyowekewa na shariah ya Kiislamu, na sio inayo tambuliwa na sheria yao inayo gongana na Shariah:

Kwa mfano, endapo mtu ataibiwa kitu, Uislamu utamrudishia mali zake zilizo ibwa; hivyo basi, inaruhusiwa kwa yule aliyeporwa kwenda mahakamani arudishiwe mali zake zilizo ibwa. 

Katika mfano mwingine, endapo mtu atauza nyumba yake kwa kianzio cha malipo, na malipo yaliyo salia kufanywa kwa mpango maalumu wa malipo, lakini mnunuzi akaishia tu kulipa kianzio hicho cha malipo pekee, na kukataa kulipa malipo yaliyo bakia au kukataa kuwa anadaiwa, licha ya kuwa alinunua nyumba hiyo na kuishi ndani yake. Katika hali hii, Uislamu utamrudishia muuzaji haki zake kutoka kwa mnunuzi huyo na hivyo basi, inaruhusiwa kwa muuzaji kwenda mahakamani ili kurudisha bei ya nyumba yake, ambayo mnunuzi amekataa.

Kwa hivyo, yaani inaruhusiwa kwake kwenda mahakamani katika Dar al-Kufr ili kuzuia ukandamizaji juu yake na kuregesha haki yake, maadamu haki hii amepewa kupitia sheria ya Kiislamu.

Kwa upande mwingine, ikiwa haki hii amepewa kupitia sheria za kibinadamu, inayo gongana na Shariah, hapo haruhusiwi kwenda mahakamani kudai haki hii inayo gongana na Shari’ah:

Kwa mfano, endapo mtu anamiliki hisa katika kampuni ya hisa, iliyoundwa juu ya mkataba batili, na wakati wa kugawanya mgao kwa wenye hisa unapowadia, mtu akagundua kwamba fungu lake katika mgao huo ni dogo kuliko vile inavyo stahili kuwa. Katika hali hii, hairuhusiwi kwenda katika mahakama za Dar al-Kufr kudai haki kamili ya hisa zake, kwani, muundo wa kampuni hii ni Batili na faida zitokamanazo nayo hazikubaliwi na Shari'ah. Hivyo basi, ni wajib juu ya Muislamu huyu kujiondoa kutoka katika muundo kama huu wa kampuni.

Katika mfano mwingine, endapo mtu ameweka pesa zake katika benki ya Riba, kwa kiwango maalumu cha riba, lakini pindi benki hiyo ilipompa fungu lake, ilifanya hesabu ya riba yake kwa kiwango kidogo kuliko kile alicho kubaliana na benki hiyo. Katika hali hii, hairuhusiwi kwenda katika mahakama za Dar al-Kufr kudai asilimia yake kamili ya Riba, na kuilazimisha benki hiyo kulipa asilimia hiyo ya Riba, kwani "haki" hii amepewa na sheria za kibinadamu, zinazo ruhusu benki za Riba, lakini si haki kwake kwa mujibu wa Shari’ah ya Kiislamu. Hivyo basi, ni Wajib juu ya Muislamu kufutilia mbali mkataba huu wa Riba pamoja na benki hiyo.

Kwa hivyo, endapo mtu atadhulumiwa au kunyimwa haki zake, na haki hizi amepewa chini ya vifungu vya Kiislamu, hapo anaruhusiwa kwenda katika mahakama za Dar al-Kufr ambako anaishi ili kujiondolea ukandamizaji huu na kuregesha haki yake. Kinyume chake, ikiwa haki hii amepewa na sheria za kibinadamu na sio vifungu vya Kiislamu, hapo haruhusiwi kwenda katika mahakama za Dar al-Kufr ambako anaishi ili kupata haki hii… Lakini, ni bora kwake kujaribu kuregesha haki yake kupitia utumiaji wa wapatanishi kutoka katika watu wa kheri kabla ya kwenda katika mahakama hizo.) Mwisho wa jibu letu lililopita. 

Nataraji hili linajibu kwa kutosheleza swali lako, na Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mjuzi zaidi na Mwingi wa hekima.

Ndugu yenu,

Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah

14 Rabii’ II 1441 H

Jumatano, 11/12/2019

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoAlhamisi, 02 Aprili 2020 20:28
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.