Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

Msururu wa Maswali Yaliyo Wasilishwa kwa Mwanachuoni Mkubwa Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah, Amiri wa Hizb ut Tahrir katika ukurasa wake wa Fiqhi wa Facebook

Swali na Jibu
Eda (kipindi cha kusubiri) ya Mwanamke Aliye poswa ambaye Mumewe Amefariki
Kwa Malek Salem na Abu Bakr Al-Fuqahaa’
(Imetafsiriwa)

Swali la Malek Salem:

Sheikh wangu, tafadhali niruhusu, niulize swali: mwanamke aliye poswa, endapo mumewe amefariki, je, ana eda? Je, atamrithi mchumba wake? Mwenyezi Mungu kulipe kheri iliyo bora.

Swali la Abu Bakr Al-Fuqahaa’:

Mwenyezi Mungu akulipe mema sheikh wetu, je, eda hutekelezwa baada ya kuingiliwa au baada ya tu kukamilisha mkataba pekee? Kwa sababu kuna visa vya talaka ambavyo hakukupatikana kuingiliwa kwa sababu moja au nyengine, hivyo je, eda ni moja katika hali zote?

Jibu:

Assalamu Alaykom Wa Rahmatullah Wa Barakatuhu,

Maswali haya mawili yanafanana, hivyo tutayajibu yote kwa pamoja, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

1. Ikiwa makusudio ya "uposi" katika swali la mwanamke ambaye ameposwa na mwanamume, na kupatikana makubaliano ya mwanzo ya ndoa lakini baadaye mkataba wa ndoa haukukamilika yaani haukukamilika ule watu wanaouita "mkataba", wala haikupatika ombi wala kukubali kuambatana na hukmu za kisheria kuhusiana na mafungamano haya… ikiwa makusudio ya uposi katika swali ni hali hii ya uposi iliyo enea katika biladi za Waislamu, yaani, makubaliano ya mwanzo juu ya ndoa lakini pasipo kuweko mkataba wa ndoa… basi hali hii haihisabiwa kuwa ni ndoa wala haihisabiwi kuwa ni uposi na yule mwanamke bado angali ni mtu wa kando kwa mposaji hivyo faragha haijuzi kwake wala haijuzi kuonyesha chochote katika uchi ('Awrah) wake mbele yake (mwanamume)… wala uposi kwa maana hii hauna athari yoyote juu ya mkataba wa ndoa katika eda au katika urathi… nk.

2. Ama ikiwa makusudio kwa mwanamke aliyeposwa katika swali la mwanamke ambaye mwenye kumposa tayari amemuoa kwa mkataba wa ndoa ya kisheria basi yeye (mwanamke) atakuwa ni mkewe kisheria juu ya mkataba wa ndoa wa kisheria wenye athari kwa mujibu wa maelezo yaliyojengwa katika vitabu vya fiqh, na tutayabainisha baadhi yake katika nukta zifuatazo kwa idhini ya Mwenyezi Mungu.

3. Mwanamke aliyefiliwa na mumewe kabla ya kuingiliwa, yaani, baada ya kufungwa juu yake mkataba wa ndoa na kabla ya kuingiliwa, mwanamke huyu huhisabiwa kuwa ni mke wa aliyekufa na eda ya kisheria kwa mumewe aliyekufa husisabiwa nayo ni miezi minne na siku kumi kwa neno lake Mwenyezi Mungu (swt):

 (وَالَّذِينَ يُتَوَفَّوْنَ مِنْكُمْ وَيَذَرُونَ أَزْوَاجاً يَتَرَبَّصْنَ بِأَنْفُسِهِنَّ أَرْبَعَةَ أَشْهُرٍ وَعَشْراً)

“Na wale miongoni mwenu wanao kufa na wakaacha wake, hawa wake wangoje peke yao miezi mine na siku kumi.” [Al-Baqarah:234], na kwa yale yaliyo pokewa na Tirmidhi na wengineo kutoka kwa Ibn Mas'ud kwamba aliulizwa kuhusu mtu aliyemuoa mwanamke na hakuishi naye na wala hakumuingilia mpaka akafa. Basi Ibn Mas'ud akasema: atalipwa mahari ya mfano wa wanawake wenzake (katika daraja) kwa ukamilifu, na eda itakuwa juu yake na atapata urathi, Ma'qil bin Sinan al-Ashaja'i akasimama kisha akasema: Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) alihukumu kwa Birwa' bint Waashiq mwanamke miongoni mwetu kwa mithili ya yale uliyo hukumu kwayo, Ibn Mas'ud akafurahi kwa hilo… Abu 'Isa amesema Hadith ya Ibn Mas'ud ni Hadith Hasan Sahih. 

Na vilevile, yeye atamrithi mumewe aliyekufa hata kama hakuwa amemuingilia kwa neno la (swt):

 (وَلَكُمْ نِصْفُ مَا تَرَكَ أَزْوَاجُكُمْ إِنْ لَمْ يَكُنْ لَهُنَّ وَلَدٌ فَإِنْ كَانَ لَهُنَّ وَلَدٌ فَلَكُمُ الرُّبُعُ مِمَّا تَرَكْنَ مِنْ بَعْد وَصِيَّةٍ يُوصِينَ بِهَا أَوْ دَيْنٍ وَلَهُنَّ الرُّبُعُ مِمَّا تَرَكْتُمْ إِنْ لَمْ يَكُنْ لَكُمْ وَلَدٌ فَإِنْ كَانَ لَكُمْ وَلَدٌ فَلَهُنَّ الثُّمُنُ مِمَّا تَرَكْتُمْ مِنْ بَعْدِ وَصِيَّةٍ تُوصُونَ بِهَا أَوْ دَيْنٍ)

“Na fungu lenu ni nusu walicho acha wake zenu ikiwa hawana mtoto. Wakiwa na mtoto basi fungu lenu ni robo ya walicho acha, baada ya wasia waliyo usia au kulipa deni. Na wake zenu watapata robo mlicho kiacha, ikiwa hamna mtoto. Mkiwa mna mtoto basi sehemu yao ni thumni ya mlicho kiacha, baada ya wasia mlio usia au kulipa deni.” [An-Nisa’:12], na kwa hadith ya ibn Mas’ud iliyo tangulia kutajwa.

4. Mwanamke aliyepewa talaka na mumewe baada ya mkataba wa ndoa na kabla ya kuingiliwa anatofautiana hukmu zake katika upande wa eda na mwanamke aliye filiwa na mumewe, ama mwanamke aliye talikiwa kabla ya kuingiliwa yeye hana eda kabisa kwa neno lake (swt):

 (يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نَكَحْتُمُ الْمُؤْمِنَاتِ ثُمَّ طَلَّقْتُمُوهُنَّ مِنْ قَبْلِ أَنْ تَمَسُّوهُنَّ فَمَا لَكُمْ عَلَيْهِنَّ مِنْ عِدَّةٍ تَعْتَدُّونَهَا فَمَتِّعُوهُنَّ وَسَرِّحُوهُنَّ سَرَاحاً جَمِيلاً)

“Enyi mlio amini! Mkiwaoa wanawake, Waumini, kisha mkawapa talaka kabla ya kuwagusa, basi hamna eda juu yao mtakayo ihisabu. Basi wapeni cha kuwaliwaza, na muwawache kwa kuwachana kwa wema.” [Al-Ahzab: 49]

Na hapa kuna hali tofauti nayo ni ikitokea kwamba kabla ya talaka na kabla ya kuingiliwa mumewe alikaa faragha naye basi faragha hii kwa baadhi ya wanazuoni wa kifiqhi (Fuqaha) imewajibisha eda vilevile na nitakutajia baadhi ya rai za kifiqhi katika maudhui ya faragha:

- Imekuja katika Al-Mughni ya Ibn Qudamah: (swala alilo sema – Mwenyezi Mungu amrehemu):- na pindi mume anapomtaliki mkewe na alikuwa ashakaa naye faragha, basi eda yake ni hedhi tatu mbali na hedhi ambayo alimtaliki ndani yake) katika swala hili kuna vigawanyo vitatu: kigawanyo cha kwanza: kwamba eda ni wajibu kwa kila aliyekaa faragha na mumewe, hata kama hakumgusa. Na hakuna ikhtilafu baina ya wanazuoni katika wajibu wake juu ya aliye talikiwa baada ya kuguswa, ama ikiwa alikaa faragha naye na hakumgusa, kisha akamtaliki, basi hakika kwa dhehebu la Ahmad eda ni wajibu juu yake. 

(Imam Ahmad na Al-Athram wamesimuliwa, kwa isnad zao kutoka kwa Zurara bin Awfa aliyesema: Makhalifa Wema walihukumu kuwa yeyote anaye shusha pazia, au kufunga mlango, basi mahari yamewajibika juu yake, na eda imewajibika juu yake. Na al-Athram pia amepokewa kutoka kwa al-Ahnaf, kutoka kwa Umar na Ali, kutoka kwa Sa'id bin al-Musayyib, kutoka kwa Umar na Zayd bin Thabit.).

Vilevile imesimuliwa kutoka kwa Makhalifa Wema na Zayd, na Ibn Umar. Na kwa haya akasema Urwah, na Ali bin Husain, na 'Ataa, na az-Zahri, na al-Thawri, na al-Awza’I, na Ishaq, na watu wa rai, na as-Shafi' katika kauli zake za zamani.

- al-Shafi’i amesema katika kauli zake mpya: hakuna eda juu yake; na neno lake (swt):

(يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نَكَحْتُمُ الْمُؤْمِنَاتِ ثُمَّ طَلَّقْتُمُوهُنَّ مِنْ قَبْلِ أَنْ تَمَسُّوهُنَّ فَمَا لَكُمْ عَلَيْهِنَّ مِنْ عِدَّةٍ تَعْتَدُّونَهَا)

“Enyi mlio amini! Mkiwaoa wanawake, Waumini, kisha mkawapa talaka kabla ya kuwagusa, basi hamna eda juu yao mtakayo ihisabu.” [Al-Ahzab: 49], na hili ni andiko (nasi), na kwa sababu liko wazi hajaguswa, basi ni mshabaha kwa yule ambaye hajakaa faragha naye (mumewe).

Na mukhtasari ni kuwa mwanamke aliye talikiwa kabla ya kuingiliwa hana eda isipokuwa ikiwa alikaa faragha na mumewe, yaani, imethubutu kwamba yeye alikutana naye chumbani na wakafunga mlango nyuma yao peke yao, basi katika hali hii, eda ni juu yake kwa mujibu wa Imam Ahmad.

Nataji jibu hili litakuwa ni lenye kutosheleza na Mwenyezi Mungu (swt) ni Mjuzi Zaidi na Mwingi wa Hekima.

Ndugu Yenu,

Ata Bin Khalil Abu Al-Rashtah

16 Dhul Qi'dah 1441 H

Sawia na 07/7/2020 M

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoAlhamisi, 16 Julai 2020 15:49
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.