Logo
Chapisha ukurasa huu

بسم الله الرحمن الرحيم

 Habari na Maoni 

Mwamko wa Afrika Unategemea Kuukumbatia Kwake Mradi wa Khilafah Kama Badala ya Ukoloni wa Kimagharibi Ambao Ndio Mzizi wa Mateso Yake

Habari:

“Makubaliano yaliyoasisi eneo huru la kibiashara barani Afrika (AfCFTA) yalitiwa saini na nchi 44,” Moussa Faki Mahamat, mwenyekiti wa tume ya AU alisema. Kuundwa kwa eneo huru la kibiashara kama eneo kubwa zaidi ulimwenguni kumejiri baada ya miaka miwili ya majadiliano, na ni mojawapo ya miradi mikuu ya AU kwa lengo la kuleta uwiano barani Afrika. Lakini, makubaliano haya bado yatahitaji kuidhinishwa katika ngazi ya kitaifa, na yatakuwa ni yenye kuanza kutekelezwa katika muda wa siku 180 zijazo. [Chanzo: gazeti la Daily Monitor] 

Maoni:

Makubaliano haya makubwa zaidi Afrika ni ya pili kwa ukubwa duniani baada ya yale ya kuundwa kwa Shirika la Biashara Duniani (WTO). Uamuzi wa kuunda AfCFTA ulitabanniwa mnamo Januari 2012 katika kikao cha 18 cha mjumuiko wa Maraisi wa nchi na serikali za AU huku majadiliano hayo yakianzishwa na AU mnamo 2015. AfCFTA ililengwa kuunda soko moja barani la bidhaa na huduma na usambaaji huru wa biashara na uwekezaji. Kwa mujibu wa AU, hii itatoa njia ya kubuniwa kwa umoja wa ushuru wa forodha barani na umoja wa ushuru wa forodha Afrika. AfCFTA huenda ikaunda soko la Kiafrika kwa watu zaidi ya bilioni 1.2 na uzalishaji jumla (GDP) wa dola trilioni 2.5 za Kiamerika. Makubaliano haya, baada ya kutiwa saini, yatasalimishwa kwa ajili ya uidhinishwaji na nchi wanachama kabla ya kuanza kutekelezwa.  

Afrika ni bara lililo barikiwa na rasilimali nyingi mno za madini pamoja na ardhi yenye rutuba, ambazo zilistahili kulinyanyua na kuliweka ngazi za juu zaidi za maendeleo ya kisiasa, kijamii na kiuchumi na ufanisi. Lakini, bara hili limezama katika umasikini na kutegemea misaada ya kigeni kutokana na uongozi mbaya na muovu wa ufujaji unaoendeshwa na ukoloni wa kimagharibi! Wakoloni hao wamelifanya mateka bara hili hadi wa leo. Wanaendelea kuchochea ghasia na machafuko barani humu kwa kutumia vibaraka wao wa kikoloni kupitia vita vya kiwakala, maabara ya majaribio, sera za masoko huru kwa bidhaa zao, baya zaidi ni kuingiza mfumo wao wa kisekula wa kirasilimali barani humu na uhuru kama kitovu chake. Kwa upande mwengine, wakoloni kupitia makampuni yao ya kimataifa chini ya kile kinachoitwa sera za uwekezaji wa moja kwa moja wa kifedha (DFID) yanajihusisha na uporaji na ulimbikizaji mkubwa wa madini kwa ajili ya maslahi yao na kuwadanganya wenyeji na mpangilio wa ugawanyaji makombo kwa msingi wa mielekeo miwili yaani sera za Jukumu la Kampuni kwa Jamii (CSR) na sera za malipo ya ada!

Katika zama zote za ukoloni wa Ulaya, Afrika ilikuwa ikifanya biashara na mabwana zake wa Ulaya. Lakini, kwa kuzuka Amerika kama dola kuu duniani ikaweka sera kama za soko huru, zilizolengwa kupambana na mkono wa Ulaya juu ya biashara barani Afrika na badala yake kutoa fursa kwa Amerika pia kujihusisha na ufujaji rasilimali nyingi za Afrika kwa gharama ya wenyeji barani humu. Hii ilipelekea nchi za Kiafrika ambazo ni tiifu kwa Ulaya kufanya biashara na Ulaya na zile ambazo ni tiifu kwa Amerika kufanya biashara na Amerika. Haya yalithibitishwa na David Luke, mshirikishi katika kituo cha sera za kibiashara za Afrika katika Tume ya Umoja wa Mataiafa (UM) ya Kiuchumi kwa Afrika (UNECA), anayetarajia kuwa AfCFTA itasahihisha “dosari ya kihistoria”. Zaidi ya hayo, aliongeza kusema kuwa, “Ukoloni ulisababisha hali ambapo majirani walikoma kufanya biashara baina yao. Njia pekee ya kibiashara ilikuwa kati ya nchi za Kiafrika na nchi za Ulaya na kati ya nchi za Kiafrika na Amerika.”

Nchi kumi na moja, zikiwemo Nigeria, Afrika Kusini, Botswana, Lesotho, Namibia, Zambia, Burundi, Eritrea, Benin, Sierra Leone na Guinea Bissau, zimekataa kujiunga/kutia saini makubaliano hayo. Zikiongozwa na Nigeria, ambayo Raisi wake, Muhammadu Buhari alionyesha kuwa matarajio ya bara hili hayaku lingana na malengo ya kitaifa ya nchi hiyo na jopo la wafanyikazi la Nigeria (muungano mkuu wa vyama vya wafanyikazi vya Nigeria) lilimuonya Buhari dhidi ya kutia saini makubaliano haya, likiyaita “mpango wa sera huru mamboleo ulioanzishwa upya, ulio hatari zaidi na wenye madhara”. Zaidi ya hayo, Waziri wa biashara na viwanda wa Zambia, Christopher Yaluma alisema katika taarifa kwamba Zambia haitatia saini makubaliano juu ya huru wa watu kutembea, kwa kuwa nchi hii haikuwa tayari kwa hilo. Thibitisho kuwa nchi zina dukuduku juu ya AfCFTA, Albert Muchanga, kamishna wa AU katika biashara na viwanda alitoa taarifa na kusema, “Baadhi ya nchi zina dukuduku na bado hazijakamilisha mashauriano yao ya kitaifa. Lakini tutakuwa na kongamano jengine nchini Mauritania mnamo Julai ambapo tunatarajia nchi zenye dukuduku pia kutia saini”.  

Kufeli kwa AfCFTA ni jambo la yakini na tayari imefichuliwa kupitia dukuduku ya mataifa mengine kwa kuwa haiendeshwi kwa aqliyya na nafsiyya huru za Kiislamu zilizo jengwa juu ya mfumo safi wa Kiislamu ulioteremka kwa wahyi kutoka kwa Muumba na ambao kipimo chake ni halali na haramu. Badala yake, imejengwa juu ya uhuru bandia kutokana na aqliyya tiifu kwa ukoloni inayo endeshwa na mfumo wa kisekula wa kirasilimali unaotumia manufaa na hasara kama kipimo cha vitendo. Mwamko wa Afrika unategemea kuukumbatia kwake mradi wa Khilafah kama badala ya ukoloni wa Kimagharibi ambao ndio mzizi wa mateso yake. Khilafah iliyo simamishwa kwa manhaj ya Mtume (saw) itadhamini amani, utulivu na ufanisi kutokana na kutekelezwa kwake mfumo wa Kiislamu na nidhamu zinazo tokamana nao kikamilifu kwa kuzitumia rasilimali zake na kuweka mipangilio inayo simamia biashara kama inavyo agizwa na Uislamu. Zaidi ya hayo, Afrika chini ya Khilafah itadhaminiwa rasilimali zake na kutumiwa kwa manufaa ya bara la Afrika, na wakoloni pamoja na makampuni yao ya kimataifa kufurushwa chini ya uongozi wa Khalifah muweza anaye shajiishwa na kupata radhi za Allah (swt). 

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Ali Nassoro Ali

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Kenya

Imebadilishwa mara ya mwisho mnamoJumapili, 09 Agosti 2020 07:01
Template Design © Joomla Templates | GavickPro. All rights reserved.